Monday, September 26, 2011

Wanawake kushiriki uchaguzi Saudia


Wanaume nchini Saudi Arabia kwa mara ya kwanza katika historia ya nchi hiyo wameruhusiwa kushiriki kwenye uchaguzi.

Mfalme wa Saudi Arabia ametoa agizo akiwaruhusu wanawake kushiriki kama wagombea kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa na Baraza la Ushauri.

Sheria za Saudi Arabia zinawazuia wanawake wa nchi hiyo kushiriki kwenye shughuli zozote za kisiasa na pia kuwa na simu za mkononi na vilevile leseni za kuendeshea magari.

Ukiukwaji huo wa haki za wanawake huko Saudia ni mkubwa kwani wanawake wa nchi hiyo hawaruhusiwi hata kuingia kwenye maeneo mengi ya umma bila ya kuwa na mawalii au wasimamizi wao wa kiume.


UN yaanza kuijadili Palestina



Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa jana limeanza kushauriana kuhusiana na ombi la Palestina kutaka uwanachama kamili wa umoja huo, ingawa kura kwa ajili ya ombi hilo haitarijiwi kufanyika mnamo majuma kadhaa yajayo.


Marekani imetishia kutumia kura yake ya turufu kupinga ombi hilo, ikisisitiza kuwa ni mazungumzo tu ya ana kwa ana kati ya Israel na Palestina ndiyo yatakayoweza kuzaliwa kwa taifa la wapalestina.

Pande nne zinazojihusisha na amani ya Mashariki ya kati, Umoja wa Mataifa, Umoja wa Ulaya, Marekani na Urusi zimekuwa katika juhudi za kutaka njia ya kuyafufua mazungumzo kati Israel na Palestina.


Bill Clinton amshambulia Netanyahu


Rais wa zamani wa Marekani, Bill Clinton, amesema Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu, ndiye aliyesababisha kukwama mwenendo wa amani ya Mashariki ya Kati.


Katika mazungumzo yake ya kidiplomasia pembezoni mwa kikao cha 66 cha Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, Clinton amesisitiza kuwa, Netanyahu ndiye anayebeba dhima ya kukabiliwa na mkwamo mwenendo wa amani ya Mashariki ya Kati.

Madai hayo ya Bill Clinton anayatoa katika hali ambayo, daima Marekani imekuwa ikiuunga mkono utawala wa wa Israel unaotenda jinai kila uchao dhidi ya wananchi wa Palestina.

Hayo yanajiri katika hali ambayo, Mahmoud Abbas Rais wa Mamlaka ya Ndani ya Palestina amewasilisha katika Umoja wa Mataifa ombi la Wapalestina la kutaka kutambuliwa nchi yao huru katika umoja huo, ambapo Marekani imetangaza wazi kwamba, itaupinga mpango huo na kwamba, itaupigia kura ya veto.


Prof Wangari Maathai afariki dunia



Mshindi wa tuzo ya amani ya Nobel kutoka Kenya, Profesa Wangari Maathai (Pichani), amefariki dunia hospitalini mjini Nairobi alikokuwa akitibiwa saratani.

Profesa Maathai, aliaga dunia juzi usiku hospitalini hapo alikokuwa anapewa matibabu.


Habari zinasema, Maathai, aliyeshinda tuzo hiyo mwaka 2004, alikuwa muasisi wa Shirika la Mazingira nchini Kenya.

Profesa Karanja Njoroge ambaye ni Mkurugenzi wa Green Belt Movement, shirika ambalo Prof Maathai alilianzisha amethibitisha kifo hicho.

Katika taarifa kwa vyombo vya habari Prof Njoroge alisema wakati wa kifo chake Wangari alikuwa na wanafamilia na marafiki.

Alisema Prof Maathai ambaye alikuwa na umri wa miaka 71, ameacha watoto watatu, wawili wakiume na mmoja wa kike.

Waasi wagundua kaburi lenye maiti 1,270 Tripoli

Ofisa wa Baraza la Mpito nchini Libya (Kulia), akiwaonyesha wapigapicha baki la sare ya gerezani ambayo imepatikana katika kaburi la pamoja la miili ya wafungwa zaidi ya 1,270 iliyogunduliwa na baraza hilo mjini Tripoli juzi. Mabaki hayo yanadhaniwa kuwa ya wafungwa waliouawa na maofisa wa usalama mwaka 1996 katika gereza la Abu Salim nchini humo.

Baraza la Mpito nchini Libya limesema kuwa, wameligundua kaburi la pamoja mjini Tripoli ambalo lina maiti 1,270.

Mabaki hayo yanadhaniwa kuwa ya wafungwa waliouawa na maofisa wa usalama mwaka wa 1996 katika gereza la Abu Salim.

Uasi dhidi ya Kanali Muammar Gaddafi ulianza kama maandamano kutaka wakili aliyewakilisha familia za wafungwa wa Abu Salim aachiliwe huru.

Uchimbuaji wa kaburi hilo la pamoja unatarajiwa kuanza hivi karibuni.

Msaada kwa mama


Watoto wakazi wa eneo la Nyang'andu kata ya Kivule Wilaya ya Ilala katika jiji la Dar es Salaam, wakielekea nyumbani kwao wakiwa wamebeba mboga za majani baada ya kutoka kununua.

Baada ya vuta nikuvute ya miaka 22, Troy Davis anyongwa


Licha ya shinikizo la mataifa mbalimbali kupinga hukumu ya kifo dhidi ya Troy Davis, Jimbo la Georgia nchini Marekani, limemnyonga kijana huyo na kuvuta hisia za wanaharakati wa haki za binadamu duniani kote.

Saa 5.00 usiku kwa saa za Marekani, Davis alichomwa sindano ya sumu na akafariki dakika nane baadaye. Dakika hizi za mwisho za Davis hazikuwa ngumu kwake tu, bali kwa dunia nzima iliyokuwa upande wake.

Davis alishuhudia umauti huku akishikilia msimamo wake wa kukataa kuhusika na mauaji ya Mark MacPhail yaliyotokea mwaka 1984.


Familia ya MacPhail na marafiki walikaa kwenye safu ya mbele wakiangalia. Msimamizi wa magereza alisoma amri ya kunyongwa, akimuuliza Davis kama alikuwa na chochote cha kusema, na Davis akanyanyua kichwa na kuangalia safu ya mbele na akatoa kauli kwamba alitaka kuzungumza na familia ya MacPhail.

Akasema kwamba licha ya hisia waliyonayo familia hiyo, yeye siye aliyemuua ndugu yao. Kwamba yeye binafsi hakuhusika na kilichotokea usiku ule MacPhail alipouawa, na kwamba yeye hakuwa na bastola.


Aliiambia familia hiyo kuwa anasikitishwa na kumpoteza mpendwa wao, lakini siyo yeye aliyechukua maisha ya mtoto, baba na kaka yao.

“Mimi sikumuua ndugu yenu, hili ni neno langu la mwisho kulitamka nikiwa hai, sikumuua MacPhail, naomba Mungu awasamehe wote waliotayari kuutoa uhai wangu kwa kosa ambalo sikulifanya, hamkuweza kuujua ukweli nikiwa hai naamini ipo siku Mungu atawaonyesha ukweli.

Hukumu hii ilikuwa kwanza itekelezwe mapema siku hiyo, lakini iliahirishwa wakati Mahakama Kuu ilipokuwa ikipitia rufani ya mwisho iliyowasilishwa na mawakili wa Davis.

Hata hivyo, baadaye Mahakama hiyo iliikataa rufaani hiyo.

Kwa zaidi ya mara tatu, hukumu hii ilikuwa imecheleweshwa kutokana na hoja za mawakili kwamba mashahidi saba kati ya tisa dhidi ya Davis, aidha walijikanganya au walipotosha ushahidi wao.

Msemaji wa Shirika la Kutetea Haki za Binadamu la Amnesty International, Laura Moye, amesema kwamba hukumu hii inafadhaisha sana.


"Tumepigwa na bumbuwazi. Tumefadhaishwa na tumekasirishwa sana kwamba Serikali ya Jimbo la Georgia imemnyonga Troy Davis licha ya kuwepo ushahidi wa kutosha unaotilia shaka kesi dhidi yake.

Kesi hii ya Davis ilizua umaarufu mkubwa duniani, ambapo maandamano kadhaa ya kupinga hukumu ya kifo dhidi yake yalifanyika.

Mataifa mbalimbali duniani yalituma maombi mbalimbali kuiasa Marekani isimnyonge Davis, moja kati ya mataifa makubwa yaliyotuma maombi ni Ufaransa.

Ombi la Ufaransa lilitanguliwa na maombi kama hayo kutoka kwa watu maarufu duniani, akiwamo Mkuu wa Kanisa Katoliki, Baba Mtakatifu Benedict wa XVI, rais wa zamani Marekani, Jimmy Carter na Askofu Desmond Tutu wa Afrika ya Kusini.


Troy Anthony Davis alizaliwa Oktoba 9, 1968. Alishtakiwa kwa kosa la kumuua Mark MacPhail mwaka 1989.

Siku ya tukio Macphail aliuawa wakati akijaribu kuamua ugomvi dhidi ya watu wawili ambao inasemekana mmoja wao alikuwa Davis.

Katika ugomvi huo mmoja wao alidaiwa kufyatua risasi (Baadaye ikadaiwa kuwa ni Davis ndiye aliyefanya kitendo hicho) ambayo ilichukua uhai wa marehemu MacPhail.

Avunja rekodi kwa kuwa na ulimi mrefu zaidi duniani



Kila kiungo katika mwili wa binadamu kimetengenezwa kwa kazi na ukubwa maalum, kuzidi au kupungua kwa kiungo kimoja umbo au ukubwa wake.

Lakini baadhi ya watu wamekuwa na viungo vikubwa au vidogo kupindukia, wengine hali hiyo huwasababishia matatizo na wengine huishi bila shida yeyote.

Chanel Tapper ameingia kwenye kitabu cha rekodi ya dunia (Guinness Book of World Records) baada ya kugundulika kuwa ndiye binadamu mwenye ulimi mrefu kuliko wote duniani.

Tapper (21), mwanafunzi katika Chuo Kikuu cha California, USA, ulimi wake unaweza kufunika pua yake pamoja na kuvuka kidevu.


Ulimi wa Tapper unakadiriwa kuwa na urefu wa Sentimeta 9.75 huku wataalam wa viungo vya binadamu wakiulinganisha na urefu wa simu ya mkononi aina ya iPhone.

Mrembo huyo anasema kuwa licha ya kuwa na ulimi mrefu, hana matatizo yoyote na mtu hawezi kumgundua mpaka atoe ulimi wake nje.

Anaongeza kuwa ana uwezo wa kula vitu vilivyopo kwenye makopo membamba kwa kutumia ulimi wake na hivyo kutohitaji kijiko.

"Nasikia ladha ya chakula kama kawaida, ila nafurahi sana pindi ninapokutana na watu nikitoa ulimi wangu nje watu wanashtuka, inanifurahisha sana,” anasema.

"Wasichana na wanawake wengine wanaruka na kukimbia na ikiwa nipo katika mkusanyiko wa watu wanaambizana na kuniafuata wakiniomba nitoe tena ulimi wangu nje,” anaongeza Tapper.


Anasema mara ya kwanza kugundulika kuwa ana ulimi mrefu kuliko kawaida, alikuwa na umri wa miaka minane.

"Tulikwenda kupiga picha kwa ajili ya kuhifadhi kumbukumbu nikiwa na mama, picha mojawapo tulitoa ulimi nje na ilipotolewa ndipo tulipogundua hilo," anasema.

Anasema wengi wamekuwa hawaamini wanapomuona na kuongeza kuwa hawezi kubadilisha maumbile yake kwani ndivyo alivyozaliwa na hapati shida ya aina yoyote kutokana na kiungo hicho.

Hata hivyo, urefu wa ulimi wa Tapper huenda ni urithi kutoka kwa mama yake.

“Mama yangu ana ulimi mrefu, lakini si kama mimi. Naamini nilizaliwa pasipo kuwa na ulimi mrefu hivi, lakini uliendelea kukua kwa kadri nilivyokua," anasema.


Kuhusu mahusiano, Tapper anasema hakuwahi kupata shida ya aina yoyote kwa wapenzi aliowahi kuwa nao, kwani waliona ni jambo la kawaida, anasema kwa sasa hayupo kwenye mahusiano.

Aliyekuwa akishikilia rekodi hiyo tangu mwaka 2006 ni Stephen Taylor, raia wa Italia ambaye alikuwa na ulimi wenye urefu wa sentimeta 9.5.

Mwaka 2001 mwanadada Annika Irmler raia wa Ujerumani alishikilia rekodi hiyo kwa kuwa na ulimi wenye urefu wa sentimita 7.

Mercy: aliuza maji mitaani, akawa ‘housegirl’ sasa ni tajiri



Kutoka Nigeria-Mercy Johnson Ozioma- aliazimia kuonyesha kipaji chake na kuvuka mipaka kadhaa mpaka Tanzania.

Na kweli hakufanya makosa. Alicheza filamu maarufu ya ‘She is My Sister’ akiwa na Monalisa na Steven Kanumba, waigizaji wa hapa nchini.

Mwigizaji huyu ambaye anasifika kwa umahiri wa kuigiza nafasi za kulia au kunyanyaswa, amefunga ndoa na mfanyabishara Prince Okojie, Agosti 27 mwaka huu.

Mercy ambaye wengi humsifia kwa umbile lake zuri na rangi nyeusi ya Kiafrika, takwimu zinamtaja kuwa ni mmoja waigizaji wanaoilipwa zaidi Nollywood. Mafanikio haya, yanamkumbusha safari ya maisha yake; alikotoka na hilo humtoa machozi.

Alizaliwa mwaka 1981 katika Mtaa wa Satellite, jijini Lagos, akiwa ni mtoto wa nne kati ya saba. Hata hivyo, hakuweza kumaliza shule kutokana na kukosa ada.

Anakumbuka jinsi familia yake ilivyohamia katika nyumba isiyokamilika. Anazivuta kumbukumbu hizo na kuona jinsi walivyohangaika kuweka mifuko na miti juu ya paa kuukuu na kuta za nyumba wakati wa mvua.


Shuleni alikuwa akifanywa mfano na walimu kutokana na sare zake chakavu zilizochanika kila mahali.

Makali ya maisha hayakuishia hapo, aliacha shule na kwenda kuuza maji barabarani. Anaonyesha makovu miguuni aliyoyapata wakati wa kukimbizana na askari wa Jiji.

Kama haitoshi, Mercy anaeleza jinsi alivyofanya kazi za ndani, ili tu ajipatie chochote kwa familia yake.
Anasema awali hakuwa na ndoto za kuwa mwigizaji, lakini alipoitazama filamu ya ‘Sharon Stone” iliyochezwa na Genevive Nnaji, alihamasika.


Filamu yake ya kwanza, ‘Moving Train” ya mwaka 2000 ndiyo iliyofungua pazia la mafanikio. Tangu wakati huo mpaka sasa Mercy amecheza filamu zaidi ya 70.

Si hivyo tu, bali ameshinda tuzo nyingi kutokana na umahiri wake na kutalii nchi mbalimbali duniani.

Anasema: wakati mwingine anapolia katika filamu huwa anakumbuka maisha yake ya nyuma, “Nikikumbuka huwa nampa Mungu utukufu.”

Moja ya filamu maarufu na bora alizowahi kucheza ni pamoja na ‘Kill the Bride’ ‘Last Kiss’ na ‘My Heart Your Home’

Mercy hapendi kuvaa mavazi ya gharama. Anaona ni bora atumie pesa hizo kuwasaidia watoto yatima na wenye shida kuliko kununua mikoba au viatu vya gharama.


Mercy anasema siri ya mafanikio yake ni kufanya kazi kwa bidii na kumuomba Mungu ambaye amempa nguvu na kipaji.

Msanii huyu, yupo katika mikakati ya kununua nyumba ambayo ataiita ‘The House of Mercy’ kwa ajili ya watoto waishio katika mazingira magumu.

Mpaka sasa Iraq bado!

Polisi nchini Iraq na wakishirikiana na Raia wema kubeba maiti iliyozungushiwa na Shuka, iliyouawa kwa kulipukiwa na bomu,katika mji wa Karbala,jana katika ofisi za kutolewa vitambulisho na pasi za kusafiria,bomu hilo liliua watu 9.

Kweli uongozi si mchezo!!

Rais wa zamani wa Zambia, Rupiah Banda, akibubujikwa na machozi huku mke wake Thandiwe (Kulia), akimwangalia baada ya kiongozi huyo kutoa hotuba yake kwa waandishi wa habari mjini Lusaka ya kuyakubali matokeo kuwa Michael Sata ni mshindi wa uchaguzi huo. Picha na AFP.

Risasi zarindima Igunga, wabunge wawili CCM, Waitara wahojiwa polisi


HALI ya usalama katika Jimbo la Igunga inazidi kuwa tete baada ya milio ya risasi kurindima usiku wa kuamkia jana katika tukio lenye utata mkubwa, huku vyama vya Chadema na CCM vikiendelea kushutumiana.

Wakati CCM) ikidai risasi hizo zilifyatuliwa na Mratibu wa Kampeni wa Chadema, Mwita Waitara, Chadema wanadai risasi hizo zilifyatuliwa na Mbunge wa Sumbawanga mjini, Aishi Hilal wa CCM.


Tukio hilo lilitokea saa 8:00 usiku wa kuamkia jana nje ya nyumba ya kulala wageni ya Misana Lodge ambapo magari mawili aina ya Toyota Landruicer na Toyota Prado yalivunjwa vioo.

Gari hiyo ya Toyota Landcuiser linaelezwa kumilikiwa na Mbunge Hilal na Prado inadaiwa kuwa ni ya Mbunge wa Viti Maalumu CCM, Ester Bulaya, ambaye CCM kinadai kuwa wafuasi wa Chadema walitaka kumteka.

Eneo lilipotokea tukio hilo ndiko ambako wafuasi wa Chadema wanalala ikiwamo kulaza magari yao yakiwamo yanayotumika katika kampeni na magari ya wabunge hao yapo katika Kituo cha Polisi Igunga kwa uchunguzi.

Naibu Kamishina wa Polisi Isaya Mngulu, ambaye ndiye Msemaji wa Polisi katika Uchaguzi Mdogo Jimbo la Igunga alithibitisha jana kuwapo kwa tukio hilo na kueleza kuwa silaha iliyotumika ni bastola yenye kipenyo cha milimita tisa.


“Hatujafanikiwa kuipata bastola hiyo lakini kutokana na maganda mawili ya risasi tuliyoyaokota eneo la tukio, inawezekana silaha iliyotumika ni bastola ya milimita 9,”alisema Mngulu.

Naibu Kamishina huyo alisema tayari watu zaidi ya 10 wamekwishahojiwa na polisi na kuandikisha maelezo yao wakiwamo Wabunge hao wawili, Waitara na walinzi watatu walioshuhudia tukio hilo lenye utata.

“Mpaka sasa hatuwezi kusema vioo vya magari yale vilivunjwa kwa kutumia risasi au mawe na hili ni moja kati ya mambo tunayoyachunguza, ikiwamo ni nani hasa aliyefyatua risasi zile,” alisema Mngulu.

Katika tukio hilo, kada mmoja wa CCM aliyekuwamo katika gari la Mbunge Bulaya aliyetajwa kwa jina la Ramadhan Twaha, alidai kuwa amejeruhiwa kwa risasi katika mkono wake wa kushoto na kutibiwa kisha kuruhusiwa.

Lakini Kamishina huyo wa polisi alisema kuwa, asingependa kuingia kwa undani kuhusu tukio hilo, ila polisi wameshaanza uchunguzi.

Kwa mujibu wa Kamishina huyo, polisi walipekua chumba anachoishi Waitara pamoja na cha dereva wa moja ya magari ya Chadema, lakini hawakukuta bastola yeyote ndani ya vyumba vyao.

Eneo kulipotokea tukio hilo ni umbali wa meta 20 hivi kutoka Hoteli ya Peak ambayo wamefikia viongozi wa kitaifa wa CCM.


Maelezo ya Bulaya


Akizungumza na Waandishi wa habari jana, Mbunge wa Viti Maalumu, Esther Bulaya alidai kuwa usiku huo alikuwa ametokea Baa ya Silent Inn akiwa na wabunge wenzake wawili akiwamo Aishi.

Mbunge alidai wakati anatokea katika baa hiyo kuelekea katika Hoteli ya Peak walikofikia viongozi wa CCM, waliona gari ya Chadema ikija mbele yao katika barabara ya lami kuelekea Peak na kuwamulika kwa taa kali.

“Wakawa wanakuja kwa speed (mwendo kasi), ikabidi tuwakwepe. Wakati tunakweoa tuligonga kibao. Baada ya tukio hilo ikabidi dereva wetu ageuze gari tukaanza kukimbilia barabara ya kuelekea Singida,” alidai Bulaya.

Alidai kuwa baada ya kuwakwepa, Waitara alitoa bastola na kufyatua risasi hewani kulishambulia gari lao huku vijana wengine wa Chadema waliokuwa wamepakiwa nyuma ya gari hilo, wakirusha mawe.

“Ikabidi mimi nimpigie simu Mbunge Aeshi kumweleza kuwa hawa watu wanataka kuniteka naye akawasiliana na polisi ambao walikuja kusaidia. Baada ya Waitara kuona kuna gari linawafuata wakakimbilia porini,” alidai.


Kwa mujibu wa Mbunge huyo, baada ya kuona Waitara na kundi lake wanafuatwa ndipo walipogeuza gari na kurudi hoteli waliyofikia na kuingiza gari lao ndani ya geti na wakati huohuo, polisi wakafika.

Mbunge huyo alidai kuwa Mwita alianza kumwinda yeye na Aeshi muda mrefu. Wengine aliodai kuwa walikuwa wanawindwa ni Mratibu wa Kampeni wa CCM, Mwigulu Nchemba na Katibu Mkuu wa UVCCM, Martin Shigella.

Alifafanua kuwa juzi kabla ya tukio hilo, aliwakamata vijana wa Chadema wakiwa na fomu walizoziandaa kwa lengo la kuorodhesha wapiga kura na kununua shahada jimboni humo, kitendo kilichomuudhi Waitara.

Mbunge Aeshi anena

Mbunge huyo aliwaambia waandishi wa habari kuwa muda mfupi baada ya kuachana na Bulaya, alipokea simu kutoka kwake (Bulaya) akimwarifu kuwa amevamiwa na alikuwa akielekea Singida hivyo aende kumwokoa.

“Kwa hiyo nilimwambia dereva ageuze gari tukaanza kuwafuata nyuma kuelekea Singida na nilipowakaribia nikampigia Esther nikamwambia niko nyuma yake na nimeshalifahamu hilo gari linalomfukuza,” alisema.

Alisema baada ya kulibana sana gari hilo liliingia porini naye akalifuata huko na ndipo likageuza kurudi mjini na yeye akaendelea kulifukuza na kwamba, akiwa njiani alikutana na polisi wa doria akawaarifu.

“Polisi nao wakatufuata hadi pale wanapokaa, lakini wanaonekana ni wajanja sana maana tulikuta gati (lango) likiwa wazi gari lao likaingia moja kwa moja hadi ndani na wakati huo polisi wakafika,” alidai.

Alidai kuwa wakiwa katika taharuki hiyo, ghafla gari yake ilipigwa kwa risasi kioo cha pembeni ambayo ilipita na kuvunja pia kioo cha upande wa pili na kwamba, tukio hilo lilishuhudiwa na polisi waliokuwa eneo hilo.

Tundu Lissu awageuzia kibao CCM

Mkurugenzi wa Sheria na Katiba wa Chadema, Tundu Lissu, alisema jana kuwa vijana wao ndio waliovamiwa na kundi la Vijana wa CCM wakiongozwa na Mbunge wa Jimbo la Sumbawanga mjini, Aeshi.

“Lengo lao lilikuwa ni kuchoma magari yetu moto, baada ya kugundulika kuwa wameingia katika eneo la hoteli tulipokaa, vijana wetu walianza kupiga kelele na kuizunguka ile gari ya Mbunge wa Aeshi,” alisema.


Lissu aliongeza kuwa baada ya mbunge huyo kuona amezungukwa alichomoa bastola na kufyatua risasi hewani watu wakalala chini akatoroka, lakini ile gari yake ilidhibitiwa hadi polisi walipokuja.

Alifafanua kuwa polisi walilichukua gari lile na kumtafuta Mbunge huyo na kumpeleka kituoni.

Lisu alisema anashangaa badala ya polisi kumkamata mbunge huyo kwa matumizi mabaya ya silaha, walimwachia huru.

“Badala ya kumweka ndani kama walivyowaweka ndani Wabunge wetu waliotuhumiwa kumvua yule Mkuu wa Wilaya kilemba cha kichwani wakawaachilia na badala yake wanakuja kumpekua Waitara,” alisema.

Alidai kuwa mtu aliyetoa taarifa polisi kuwa Waitara ana silaha ni Mbunge Esther Bulaya aliyekuwepo pia kwenye tukio hilo la saa 8:00 usiku na kumtuhumu kwa kuwatukana polisi alipofika kituo cha polisi Igunga.

“Yule mbunge aliyefyatua risasi yupo huru bunduki yake anayo… na Rage (Ismail) aliyekuwa na bunduki juzi kwenye mkutano wa hadhara yupo huru licha ya makatazo ya tume ya uchaguzi…,”alilalamika.

Alisema jeshi la polisi linatumika kama chombo cha mabavu badala ya kutumika kama chombo cha kulinda amani na kwamba, wakiambiwa wakamate watu wa Chadema wanawakamata bila kuuliza.

Waitara azungumza

Kwa upande wake, Mwita Waitara alisema anashangazwa na hatua ya Mbunge Bulaya kumsingizia tukio kubwa kama hilo.

Aliwaambia Waandishi wa habari kuwa wakati wa tafrani hiyo yeye alikuwa amelala chumbani kwake na alishtuka usingizini kutokana na kelele alizozisikia nje.

Waitara alisema pamoja na yeye kutokuwapo kwenye gari usiku huo, anashanagzwa na hatua ya polisi kumkamata na kumshikilia kwa saa kadhaa.

Chadema wataka mgombea

CCM aenguliwe

Lissu alisema tayari Chadema kimemwandikia barua Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili ya Uchaguzi kulalamikia kitendo cha Mbunge wa Tabora mjini, Ismail Aden Rage, kutembea na bastola waziwazi hadharani.

Kutokana na kitendo hicho, Chadema kimemwomba mwenyekiti wa kamati hiyo ya maadili kukiomba mgombea wa CCM, Dalaly Kafumu, aondolewe kwenye kampeni kutokana na ukiukwaji huo wa maadili.


Lissu alisema Ibara ya 2(2) ya Maadili ya Uchaguzi ya mwaka 2010 ilivyofanyiwa marekebisho Septemba 20, mwaka huu inakataza kubeba silaha yoyote inayoweza kudhuru mtu yeyote katika mikutano ya kampeni.

Alilitaka Jeshi la polisi kumkamata Rage na wabunge waliofyatua risasi na kuwaweka rumande akisema kama hilo litafanyika ataamini jeshi hilo linatenda haki kwa usawa na bila upendeleo.

Polisi kumhoji Rage

Naibu Kamishina wa polisi, Mngulu alisema polisi watamhoji Mbunge wa Tabora Mjini Aden Rage kwa kitendo chake cha kutembea na bastola hadharani.


“Tutaanza kwa kumhoji Mheshimiwa Rage kwa nini alitembeza na bastola na uchunguzi utakapokamilika tutatuma kwa wataalamu wa sheria ili wafanye ufafanuzi kwamba katika hali ile inakuwaje,” alisema.

CCM nao watoa tamko

Katibu wa NEC Fedha na Uchumi, Mwigulu Nchemba alisema jaribio la kutaka kutekwa kwa wabunge wao wawili usiku wa kuamkia jana ni mwendelezo wa matukio ya vurugu dhidi ya wana-CCM na viongozi wake.

Nchemba alisema yeye na wabunge hao wamekuwa wakiwindwa kwa muda mrefu na Chadema baada ya wao kubadilisha upepo na kuwafanya vijana wabadilike na kuamua kukiunga mkono CCM.

Katibu huyo ambaye pia ni mratibu wa kampeni za CCM jimbo la Igunga amelaani tukio hilo na matukio mengine, akiwataka polisi kuwakamata wote waliotajwa kuhusika kuwashambulia wabunge hao.


Zitto Kabwe atua Igunga

Katika hatua nyingine Mbunge wa Kigoma Kaskazini Zitto Kabwe, jana aliingia katika Jimbo la Igunga kuongeza nguvu ya kampeni kwa chama chake cha Chadema na kupata mapokezi makubwa kutoka kwa wanachama na wapenzi wa chama hicho.