Tuesday, November 29, 2011

Mvua yaleta maafa Arusha


Mvua kubwa ya upepo iliyonyesha usiku wa kuamkia jana imesababisha mafuriko makubwa, maporomoko ya mawe kwenye Mto Kirurumo uliopo mpakani mwa Wilaya mbili za Karatu na Monduli, mkoani Arusha.

Kutokana na mvua hizo mtu mmoja amefariki dunia na mwingine kujeruhiwa baada ya kuzolewa na maji kilomita nne ambako maiti yake iliokotwa.

Mbali na kifo na majeruhi huyo, mvua hizo pia zimewaacha mamia ya wakazi wa maeneo hayo bila makazi kutokana na nyumba kadhaa kusombwa na mafuriko hayo.



Watalii, wagonjwa wakwama

Idadi kubwa ya watalii, ambao jana walitarajia kuendelea na safari kwenda Hifadhi za Serengeti na Ngorongoro na wengine kurejea Arusha walikwama katika barabara hiyo na kubaki wamekaa kwenye magari.

Mmoja wa watalii hayo, Johnson Taylor kutoka Uingereza alisema alikuwa ametarajia kuwahi Arusha jana ili kusafiri kurejea nchini kwao, lakini amekwama.

“nimefika hapa tangu saa 12:00 asubuhi, lakini tumeshindwa kupita kutokana na barabara kuharibika…hii ni tatizo kubwa sasa tunafanya mawasiliano kuona kama tiketi za safari zitabadilishwa”alisema Taylor.



Wananchi waombwa

kuhama mabondeni


Mbunge wa jimbo la Karatu, Mchungaji Israel Natse na mkuu wa wilaya hiyo, Methew Sadoyeka walitoa wito kwa wananchi ambao wanaishi katika maeneo ya mabonde kuhama sasa kwani taarifa za utabiri wa hali ya hewa zimesema kutakuwa na mvua nyingi hadi Desemba.


JWTZ waenda kufungua barabara

Askari wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi (JWTZ), kutoka Makao Makuu ya Brigedi ya Mbuni wilayani Monduli, jana walifika eneo la tukio Mto wa Mbu kusaidia kazi ya kufungua barabara ya Karatu-Arusha ili kuruhusu magari kupita.


Rais Bashir amtimua balozi wa Kenya


RAIS Omar al-Bashir wa Sudan amemfukuza Balozi wa Kenya nchini humo, kufuatia Mahakama Kuu ya Kenya kutoa amri ya kukamatwa kwa rais huyo. Pia amemuagiza balozi wake aliyeko mjini Nairobi arejee nyumbani.

Rais Bashir ambaye anatafutwa na Mahakama ya Uhalifu ya Kimataifa (ICC) amempa saa 72 balozi huyo awe ameondoka mjini Khartoum.

Kwa mujibu wa Jaji wa Mahakama Kuu ya Kenya, Nicholas Ombija, Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Waziri wa Usalama wa Ndani lazima watekeleze amri hiyo ya kumkamata iwapo Rais Bashir atakanyaga tena ardhi ya Kenya.



Habari zinasema, japokuwa Kenya ni mwanachama wa mahakama ya ICC, vyombo vyake vya usalama havikuweza kumkamata Rais Bashir wakati alipoitembelea Kenya mwezi Agosti, mwaka jana.

Kutokana na hatua hiyo, baada ya tawi la shirika lisilo la kiserikali, Tume ya Kimataifa ya Wanasheria, iliomba Mahakama Kuu itoe hati ya kumkamata. Wizara ya Mambo ya Nje ya Sudan awali ilijaribu kupuuza uamuzi wa Jaji huyo ikisema uamuzi huo ulikuwa ni maswala ya ndani ya Kenya, ambayo yasingeathiri uhusiano kati ya Sudan na Kenya.