Monday, January 30, 2012

Dk Mwakyembe ajitokeza hadharani, arusha kombora


Hatimaye, Naibu Waziri wa Ujenzi na Mbunge wa Kyela, Dk Harrison Mwakyembe jana alijitokeza hadharani na kusema amepona huku akiapa kuendeleza vita dhidi ya mafisadi hadi kifo chake.

Dk Mwakyembe aliondoka nchini Desemba 9, mwaka jana kwenda katika Hospitali ya Appolo, India kwa matibabu baada ya kuugua maradhi yaliyosababisha ngozi yake kuharibika na tangu arejee alikuwa hajawahi kuonekana katika hadhara ya watu.

Jana, waziri huyo alionekana mwenye afya njema huku akiwa amevalia suti, glovu nyeusi na kofia aina ya pana.

Akiwa na kundi la makada wenzake wa CCM wanaojipambanua kupambana na ufisadi, akiwemo Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samwel Sitta, Dk Mwekyembe alisema awali, alikuwa na hali mbaya kiafya lakini sasa anamshukuru Mungu kwa kuwa anaendelea vizuri.

Mwakyembe na kundi hilo walikuwa katika uzinduzi wa Programu ya Neno la Hekima kutoka kwa Kiongozi iliyoanzishwa na Kanisa la Ufufuo na Uzima na kuongozwa na Mchungaji Josephat Gwajima, Dk Mwakyembe.

Wengine waliohudhuria ni Mbunge wa Same Mashariki, Anne Kilango Malecela, Mbunge wa Kahama, James Lembeli, Mbunge wa Viti Maalumu Mbeya, Hilda Ngoye, aliyekuwa Mbunge wa Vunjo, Aloyce Kimaro na Mjumbe wa Umoja wa Vijana (UVCCM), Mkoa wa Kilimanjaro , Paul Makonda.


Mbali ya kuapa kuendeleza mapambano dhidi ya mafisadi, Dk Mwakyembe pia alitoboa siri ya afya yake akisema: “Nilifika hospitalini Oktoba 10 (mwaka jana), na tangu wakati huo sikuweza kuvaa viatu lakini leo hii naweza kuvaa viatu, kwa hiyo shetani ameshindwa.”

Alisema atatumia siku za Jumapili kuzunguka katika makanisa mbalimbali kwa lengo kumkemea shetani.

Sitta atoa tuhuma

Kwa upande wake, Sitta ambaye ni mshirika wa karibu kisiasa wa Dk Mwakyembe alirejea kauli yake ya awali kuwa Naibu Waziri huyo alilishwa sumu.

“Nasema Dk Mwakyembe kapewa sumu. Kama vyombo vya uchunguzi vinasema siyo basi watueleze ukweli, tena haraka” alisema Sitta na kushangiliwa na maelfu ya waumini wa kanisa hilo.

“Vipi uone binadamu ambaye ukimshika katika ngozi unga unamwagika chini, mhudumu anakuja kuufagia lakini baada ya saa moja unarudi tena, kitu hicho siyo cha kawaida. Wamejaribu, wameshindwa kwa kuwa Dk Mwakyembe analindwa kwa jina la Yesu ambalo ni kubwa kuliko yote. Kwa hiyo nuksi, kurogwa kuwekewa sumu ni kama maji katika mgongo wa bata, yanatiririka tu na kwenda zake,” alisema Sitta.

Alisema mafisadi wapo kwa ajili ya kuangamiza taifa na kuwaangamiza viongozi wanaotetea maslahi ya wananchi na kutokana na hali hiyo, siku zao zina hesabika.

“Mungu yupo kwa ajili ya kutetea wanyonge na si kuwalinda mafisadi hao... ndiyo maana Dk Mwakyembe amepona. Kwa sababu alikuwa miongoni mwa watu wanaotetea maslahi ya wananchi,” alisema.

Tumejipanga

Kwa upande wake, Kilango alisema kundi lao la wapiganaji na wapambanaji wa ufisadi lipo makini kutetea maslahi ya taifa na si watu wachache akisema wamejitoa muhanga kwa ajili ya kuwashughulikia.

“Kundi letu limeundwa kwa ajili ya kutetea maslahi ya Watanzania, ndiyo maana tulikuwa na nguvu kwenye Bunge la Tisa la kasi na viwango ambalo lilikuwa linafanya uamuzi wa haki bila ya kumuonea mtu, kutokana na hali hiyo tumejipanga upya, tutawashughulikia,” alisema.

Alisema Bunge hilo lililoongozwa na Sitta lilikuwa makini kwenye uamuzi na kwamba hawataogopa kulishwa sumu wala kutishiwa maisha akisema wako tayari kwa lolote kwa ajili ya kutetea maslahi ya wananchi na wana imani kwamba watashinda.

Naye Lembeli alisema Mungu amemponya Dk Mwakyembe na sasa yuko tayari kufa kwa ajili ya kutetea maslahi ya wananchi huku Ngoye akisema amezaliwa ili kutetea maslahi ya wananchi na kupambana na walafi, wala rushwa na mafisadi wanaodhulumu haki za wananchi.

“Tumerudi kwa kishindo, kwa ajili ya kutetea haki zenu, tunaomba mzidi kutuombea ili tuweze kuwashughulikia, hatuwezi kuona wananchi wananyonywa na wachache wakati wenyewe wananeemeka,” alisema Ngowe.

Kwa upande wake, Kimaro alidai kwamba mafisadi walitumia zaidi ya Sh120 milioni kwa ajili ya kumng’oa jimboni kwa sababu alionekana ni miongoni mwa watu wanaojifanya wana kimbelembele katika kutetea maslahi ya taifa.

Alisema licha ya kutoka bungeni, msimamo wake utabaki palepale, kutetea maslahi ya wa wananchi na Watanzania kwa ujumla... “Haiwezekani rasilimali za Watanzania ziliwe na wachache. Tutapambana iwe kwa jua au mvua,” alisema Kimaro.


Madaktari waendeleza libeneke

Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Dk. Haji Mponda, Waziri wa Mambo ya Ndani Shamsi Vuai Nahodha na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam wakiwa busy na simu zao Muhimbili jana, wakiwa katika harakati za kunusuru mgogoro ili madaktari warejee kazini.

Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Dk. Haji Mponda, Naibu wake Dk. Lucy Nkya (kushoto) na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Hawa Ghasia (kulia) wakijadili jambo kabla ya kutambulisha katika mkutano wa madaktari katika hoteli ya Starlight kabla ya kutimuliwa kikaoni hapo.

Tuesday, January 24, 2012

Women In Balance-kitchen party Gala

Mratibu wa wa Wanawake Mezani (Women In Balance-kitchen party Gala), Dina Marios akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana , kuhusu msimu wa pili wa mkusanyiko wa wanawake waliolenga kutoa mafunzo kwa wanawake wenzao katika Nyanja mbalimbali za kijamii utakaofanyika Jumamosi Mikocheni jijini Dare s Salaam. Kulia ni Mratibu, Vida Mdolwa.



Kwaheri mdogo wetu Beatus Kagashe


Viongozi wa MCL, ndugu na jamaa wakiliingiza jeneza lenye mwili wa marehemu Beatus kanisani tayari kwa maombi na sala ya kumwaga


Marehemu Beatus Kagashe



Kumwelezea marehemu
Mama wa marehemu akimwelezea mwanaye

Mhariri Mtendaji wa mwananchi Communication

Mke wa marehemu (kulia)





Ni kweli huu ndio mpira wa Bongo??!!


Niliuona huu mchoro uliyochorwa na kaka yangu Sammy kwenye gazeti la Citizen, ulinifurahisha sana. lakini ndio hali halisi, Tanzania hatuna timu, kazi yetu kuchezesha mpira kwa midomo yetu na magazetini.

Thursday, January 19, 2012

Tanzania yawakilisha dai la nyongeza eneo la bahari


Jahhuri ya Muungano wa Tanzania, imewasilisha katika Umoja wa Mataifa, Andiko la kudai eneo la nyongeza lenye ukubwa wa maili 16,000 nje ya eneo la sasa la maili 200 za Ukanda wa Kiuchumi wa Bahari.

Waziri wa Ardhi na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Anna Tibaijuka (Mb) ndiye aliyewasilisha Andiko hilo, kwa niaba ya serikali, katika hafla fupi na ya kihistoria iliyofanyika siku ya Jumatano katika Ofisi za Idara ya Umoja wa Mataifa inayoshughulikia masuala ya Bahari na Sheria ya Bahari.

Andiko hilo lilipokelewa na Mkurugenzi wa Idara hiyo, Sergei Tarassenko kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ambaye aliipongeza Tanzania kwa hatua hiyo muhimu na kuahidi kwamba Idara yake kupitia, Kamisheni ya Umoja wa Mataifa inayohusika na mipaka ya bahari italifanyia kazi andiko hili.

Mkurugenzi huyo alielezea Tanzania, kama moja kati ya nchi inayoheshimu na yenye historia nzuri katika Umoja wa Mataifa.

Akizungumza wakati wa kuwasilisha Andiko hilo, Waziri Anna Tibaijuka, alisema kwa kuwasilisha Andiko hilo, Tanzania si tu kwamba imefanya kazi ya uhakika ya maandalizi na hatimaye uwasilishaji lakini ni hatua kubwa kwa maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa Tanzania.

Waziri wa Ardhi na Maendeleo ya Makazi , Anna Tibaijuka akimkabidhi Mkurugenzi wa Idara ya Umoja wa Mataifa ya Masuala ya Bahari na Sheria ya Bahari, Sergei Tarassenko kwa Niaba ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, andiko la kudai nyongeza ya maili 61,000 nje ya eneo la maili 200 la Ukanda wa Kiuchumi wa Bahari , jijini New York, Marekani.

Akabanisha kwamba mchakato wa maandalizi ya Andiko hilo ambao umechukua miaka mitano, umewashirikisha wataalamu mbalimbali wakiwamo wa ndani na nje , ikiwa ni pamoja na kuzihusisha nchi ambazo zinapakana kibahari na Tanzania.

Akizungumza manufaa ya kudai nyongeza ya eneo hilo, Waziri Tibaijuka alisema. “ Tanzania itanufaika kwa kuongeza ukubwa wa eneo la mipaka ya nchi lakini la msingi zaidi ni unufaikaji wa rasilimali zikiwamo za mafuta na gesi na madini ambazo zitakuwamo katika eneo hilo jipya, rasilimali ambazo kwa sasa zinaelekea kutoweka katika eneo la maili 200”.

Eneo ambalo Tanzania inadai liongezwe la maili 61, 000 ukubwa wake ni sawa na eneo la mikoa mitatu ikiunganishwa kwa pamoja.

Aidha kuongezwa kwa eneo hilo kutaisaidia pia serikali katika masuala ya ulinzi na usalama hasa katika kipindi hiki ambacho vitendo vya kiharamia wa baharini vikiwa vimeongeza katika eneo la bahari ya Hindi.


Sunday, January 15, 2012

Mbunge Chadema afariki


Mbunge wa Viti Maalumu kwa tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Regia Estelatus Mtema (32), amefariki dunia baada ya gari alilokuwa akiendesha, kupinduka eneo la Mlandizi, Kibaha mkoani Pwani jana.

Ajali hiyo ilitokea saa 5:30 asubuhi karibu na Sekondari ya Ruvu, wakati mbunge huyo na watu wengine saba, wakisafiri kwa gari aina ya Toyota Landcruiser wakitoka Dar es Salaam kwenda Morogoro.

Akielezea mazingira ya ajali hiyo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Ernest Mangu, alisema mbunge huyo alifariki baada ya gari hilo alilokuwa akiendesha mwenyewe, kuacha njia na kupinduka.


Alisema ajali hiyo ilitokea baada ya Mtema kujaribu kulipita gari lililokuwa mbele yake na ghafla aliona gari lingine likija kasi mbele yake, katika kujaribu kulikwepa, ndipo gari hilo lilipinduka.

"Wakati akiwa hajalipita gari hilo aliliona gari lingine likija mbele kwa kasi , katika kulikwepa wasigongane uso kwa uso, alitoa gari lake barabarani na kusababisha kupinduka,’’ alisema Mangu.

Alisema watu wengine saba waliokuwa kwenye gari hilo walijeruhiwa, wawili kati yao hali zao zilikuwa mbaya, walipelekwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) Dar es Salaam kwa matibabu zaidi, huku wengine watano, wakiwahishwa Hospitali Teule ya Tumbi Kibaha.

Aliwataja majeruhi waliolazwa Tumbi kuwa ni Lawrence Mtokambali (58), Benadetha Mtema (50), Peter Madesa (50) na Rogers Abdallah(18).


Chadema yatoa tamko

Chadema kilisema kuwa Mtema alikuwa Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama hicho na Waziri Kivuli wa Kazi na alikuwa mchapa kazi hodari katika majukumu mbalimbali yakiwepo ya kijamii na kisiasa.

Taarifa hiyo iliyotolewa na Chadema jana na kusainiwa na Katibu Mwenezi wa chama hicho, John Mnyika ilieleza kuwa viongozi wakuu wa chama hicho wakiongozwa na Mwenyekiti wao Freeman Mbowe, Katibu Mkuu, Dk Willibroad Slaa, wajumbe wa Kamati Kuu, Wakurugenzi wa chama hicho makao makuu na wabunge, wameshtushwa na kifo hicho na kuungana na familia ya marehemu katika kipindi hiki kigumu cha majonzi.

Chadema kimesema taarifa zaidi kuhusu taratibu za maziko, itatolewa mara baada ya kukamilisha majadiliano kati familia ya marehemu, chama na Ofisi ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Kufuatia kifo hicho, mkutano wa Chadema uliokuwa umepangwa kufanyika jana Mjini Kibaha umehirishwa hadi itakapotangazwa wakati mwingine.



Elimu yake

Mtema alizaliwa Aprili 21, 1980. Alisoma elimu ya msingi kati ya mwaka 1989 na 1995. Alijiunga na Shule ya Sekondari Forodhani, Dar es Salaam mwaka 1996 hadi 1999 na kuhitimu kidato cha nne.

Aliendelea kidato cha tano 2002 na sita kati ya mwaka 2000 na 2002 katika Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Machame, mkoani Kilimanjaro.

Mwaka 2003 hadi 2006 alisoma Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUA) na kupata Shahada ya Maarifa ya nyumbani na Lishe.

Baada ya kuhitimu shahada yake, marehemu Mtema alifanya kazi katika taasisi mbalimbali kabla ya kujiunga na Chadema na kuteuliwa kuwa Ofisa Mwandamizi katika Kurugenzi ya Vijana ya chama hicho.

Baadaye aliteuliwa kuwa Ofisa Mwandamizi katika Kurugenzi ya Mafunzo ya chama hicho, nafasi ambayo aliishikilia hadi mwaka 2010 alipoteuliwa kuwa Mbunge wa Viti Maalum.


JK amtumia rambirambi Mbowe

Wakati huo huo, Rais Jakaya Kikwete amemtumia salamu za rambirambi Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe kufuatia kifo cha mbunge huyo.

Katika salamu hizo, Rais ameelezea kusikitishwa kwake na taarifa za kifo cha mbunge huyo na kueleza kwamba, marehemu Mtema amepoteza maisha akiwa kijana na kwamba pigo hilo si kwa Chadema pekee bali kwa taifa zima.

“Nimepokea kwa masikitiko na huzuni nyingi habari za kifo cha Mheshimiwa Mtema katika ajali ya gari. Siyo kwamba ajali hii imechukua maisha ya kijana bali imelinyang’anya taifa mbunge hodari, na kwa hakika, kifo chake siyo tu ni pigo kwa chama chako bali ni pigo kwa sote na kwa taifa letu kwa jumla.

"Nakutumia wewe binafsi, chama chako na wanachama wake salamu za dhati ya moyo wangu kuomboleza kifo na msiba huu mkubwa," alisema Rais Kikwete kupitia taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu.

Aliongeza: “Napenda ujue kuwa niko nanyi katika msiba huu. Napenda vilevile uniwasilishie salamu zangu za rambirambi za dhati kabisa kwa wana-familia, ndugu na jamaa wa marehemu Mheshimiwa Mtema.

Taarifa hiyo imemwomba Mbowe kufikisha salamu za Rais Kikwete kwa familia ya mbunge huyo na kuijulisha kuwa amepokea habari hizo kwa huzuni kubwa.

"Wajulishe kuwa nawaombea kwa Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema, awajalie uvumilivu na subira katika kipindi hiki kigumu kwa sababu yote ni mapenzi yake.





Ajali ya meli, Watu 70 wapotea, nahodha wa meli akamatwa


Wakuu wa forodha nchini Italia wamesema watu 70 wamepotea, baada ya meli ya abiria iliyobeba watu zaidi ya 4000 kwenda mrama katika mwambao katika Visiwa vya Tuscany nchini humo.

Meli hiyo ya abiria iitwayo Costa Concordia iligonga mwamba baharini na kusababisha tundu la mita 70 hadi 100 katika eneo lake la mbele, muda mfupi baada ya kuanza safari yake Ijumaa kutoka bandari ya Civitavecchia karibu na mji wa Roma.


Kikosi cha majanga kikiingia katika meli hiyo kuokoa abiria

Zaidi ya watu 42 wamejeruhiwa, ambao watu watatu hali zao ni mbaya na wengine 70 ambao ni miongoni mwa watu waliokuwa ndani ya meli hiyo hawajulikani walipo.

Meli hiyo ambayo ilikuwa imebeba abiria na wafanyakazi wapatao 4,000 ilipinduka upande mmoja. Hata hivyo, waokoaji nchini humo wanaendelea na juhudi za kutafuta watu waliopotea, baada ya meli hiyo ya abiria kupinduka.

Manrino Giampedron (57), mtumishi wa meli hiyo naye alikuwa miongoni mwa walionusurika, yeye alikuwa wa tatu kuokolewa na inasadikiwa alivunjika mguu wake mmoja

Mkuu wa kazi za uokoaji alisema hawawezi kuthibitisha idadi ya watu waliopotea kutokana na hali ya taharuki iliyopo iliyosababishwa na ajali hiyo. Hata hivyo, wakuu wa forodha nchini humo wanakadiria watu 70 wamepotea.

Habari zinasema kuwa, abiria mmoja alisema kuwa walikua wajitayarisha kwa chakula cha usiku waliposikia kishindo kikubwa kabla ya meli hiyo, kutikisika na kusimama na taa kuzimika.













Kile kibox (black box) kilipatikana, hiki ndicho kitakachotoa uhakika wa kujua ajali hiyo ilisababishwa na nini

Hii ni sehemu ya chini ya meli inavyoonekana ilivyoharibika baada ya kugonga mwamba huo, hapa linaonekana jiwe likiwa bado limeng'ang'ania sehemu hiyo hata baada ya kuitoboa.

Hapa anaonekana raia akishangaa

Uokoaji ulikuwa wa hali ya juu, hapa waokoaji walitumia helkopta pia

Nahodha akamatwa

Wakati huohuo, vyombo vya habari nchini humo jana vimeripoti kuwa nahodha wa meli hiyo, amekamatwa wakati uchunguzi unafanyika juu ya madai ya kuua bila kukusudia na kuitelekeza meli yake.

Nahodha wa meli hiyo, Francesco Schettino akiwa mikononi mwa polisi

Mkuu wa kampuni inayomiliki meli hiyo, Gianni Onorato, alisema ushahidi wa awali unaonyesha kuwa meli iligonga mwamba kisha nahodha kwa haraka akafuata utaratibu wa kuwatoa abiria melini.


Friday, January 6, 2012

Twende tukaone maajabu Rubondo


Ninashawishika kuwaalika watanzania wenzangu kwamba twendeni tukaone maajabu katika hifadhi inayoundwa na visiwa 11. Hii ni nyingine bali ni hifadhi ya Rubondo iliyopo wilaya ya Geita Mkoani Mwanza, ikiundwa na visiwa ambavyo ni

makazi ya ndege na wanyama wa aina mbalimbali.

Kwa namna vinavyoonekana, Rubondo ambayo iliyoanzishwa Januari 1977, inafananishwa na lulu ya kijani ndani ya ziwa Viktoria.

Inafikika kwa boti kupitia kituo cha Nkome wilayani Geita au Muganza upande wa wilaya ya Chato mkoani Kagera.

Awali kisiwa kilikaliwa na jamii ya Wazinza na kumbukumbu ipo eneo la 'Maji Matakatifu' yaliyotumika kwa tambiko la kupata baraka za miungu na samaki walipendelea eneo hili kuliko sehemu nyingine.


Wapo wanyama wa asili na baadhi hawapatikani katika hifadhi nyingine kama aina ya nzohe'statunga' huku hifadhi ikiwa na historia ya kuwa na uoto wa asili mithili ya misitu ya Kongo.


Moja ya matukio ya kushangaza ni ufundi wa baadhi ya wanyama ambao huogelea mpaka visiwa vingine vya hifadhi na baadhi hugeuka chakula cha wanyama wengine waishio majini.

Mkuu wa hifadhi Herman Batiho anasema mbali na kujivunia hazina ya wanyama kama tembo, twiga, viboko na mbega pia ni sehemu pekee unapoweza kuwaona kasuku wa kijivu kutoka Afrika Magharibi.

Ni eneo pekee ndani ya ziwa Viktoria linalotunzwa kwa ajili ya mazalia ya samaki.

Changamoto za kimazingira zinaongeza umuhimu wa sehemu hii kwa ajili ya maendeleo ya kiuchumi yanayotegemea rasilimali za ziwa.


Kubadilika kwa ubora wa maji ni dalili ya kubadilika kwa ikolojia ya ziwa ambapo matokeo ya Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi (Tafiri) mwaka 2009 sangara walipungua kutoka tani 750,000 mwaka 2006 hadi 227,365 mwaka 2010.


Ujangili mkubwa sio wa vipusa vya faru na tembo kama hifadhi ya Serengeti bali uvuvi wa sangara na watoto wao.

Mkuu wa hifadhi hiyo anasema ulinzi umeimarishwa kwa ajili ya usalama wa viumbe waliopo.


Kuelekea Kisiwa cha ndege

Safari ya kukifikia kisiwa cha ndege inapitia visiwa kadhaa ambavyo vina kila aina ya vivutio ukiwemo mwamba mkubwa ambacho ni kituo maalumu kwa ajili ya malezi ya watoto wa mamba.

Mayai huanguliwa kisiwa jirani na watoto husafirishwa kinywani hadi kwenye mwamba kuwakinga na maadui.


Baadhi hufa wakati wa safari na wachache hulindwa dhidi ya ndege hadi hatua ya kujitegemea.

Kisiwa cha Chambuzi kinapambwa na maelfu ya ndege kutoka Mashariki ya mbali, Afrika na Ulaya ambao hukimbia usumbufu utokanao na shughuli za binadamu na msimu wa baridi kali.


Kwa mujibu wa Christina Kibwe, mtaalamu wa ikolojia katika hifadhi ya taifa ya kisiwa cha Rubondo ni eneo pekee unapoweza kuona aina zaidi ya 200 za ndege na maelfu ya viota vyao vilivyochimbwa ardhini.


Hata hivyo ni vigumu kumuona ndege aina ya domo kiatu ambaye yuko katika kundi la vivutio vinavyotoweka na hupendelea maeneo ya ardhi oevu, kando ya mito na mabwawa.


Domo ni aina ya ndege wanaojulikana kitaalamu kama ‘balaeniceps rex’ na yuko hatarini kutoweka baada ya makazi yake kuharibiwa. Chakula chake kikuu ni samaki aina ya kambale na kamongo ambao huwasubiri waibuke.

Mtafiti katika Idara ya Zuolojia na uhifadhi wa viumbepori Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Jasson John anakiri ndege huyo atapotea katika uso wa dunia kama hatua za kumnusuru hazitachuliwa sasa.

Anasema ni kivutio kikubwa na hapa nchini wanakadiriwa kubaki ndege 200 ambao inabidi walindwe kwa mujibu wa sheria za wanyamapori na kuwa wapo ndege kati ya 5,000 na 8,000 waliobaki duniani.


Utafiti wa Mradi wa Mazingira wa Rufiji wa mwaka 2003 unatetea maarifa ya kimila na kisayansi kulinda viumbe hai. Mathalani wakazi wa maeneo hayo waliamini nyama ya kiboko hailiwi kwani hurutubisha maziwa kwa kinyesi.

Maarifa ya kimila mbali na kuokoa vizazi vya wanyama wa asili kama ilivyo katika hifadhi ya Rubondo, pia yamesaidia kuhifadhi maelfu ya hekta za misitu iliyoaminika kuwa makazi ya mizimu wakiogopa kuikasirisha kwa kuchoma moto.


Uhusiano na vijiji jirani

Utulivu wa ziwa uliniwezesha kusafiri bila shida katika boti ndogo hadi kijiji cha Nyabugela baada ya siku tatu za kutembelea visiwa vilivyozunguka hifadhi ya taifa Rubondo.

Vijiji jirani mbali na kufaidika na utalii pia vinaweza kusaidia utekelezaji wa sheria namba 5 ya mwaka 2009 inayozuia usafirishaji wa wanyama hai na kufanikisha mipango ya kudhibiti wizi wa rasilimali ambapo sekta ya utalii inachangia asilimia 17.2 ya pato la taifa.

Thursday, January 5, 2012

Urefu unamnyima gari bomba



Peter Crouch ni mshambuliaji wa Stoke City na kikosi cha England.
Akiwa na urefu wa futi 6 na inchi 7 anaaminika kuwa mchezaji mrefu zaidi kwenye Ligi Kuu England.
Crouch, ambaye alizaliwa Januari 30, 1981, alianzia soka yake katika timu ya watoto wa Tottenham Hotspur.
Hakupata nafasi katika kikosi cha kwanza cha timu ile na mwaka 2000 aliondoka na kujiunga na timu nyingine za Ligi Kuu.

Alichezea timu za Portsmouth, Aston Villa, Southampton na Liverpool kabla ya kurejea Tottenham mwaka 2009.
Ana utajiri wa kiasi cha pauni 15 milioni (Sh. 36.4 bilioni) na jumba la thamani la pauni 5 milioni (Sh 12.1 bilioni) katika eneo la Cheshire jijini Manchester.
Alinunua jumba hilo kutoka kwa nyota wa Kriketi wa England, Andrew ìFreddieî Flintoff.
Nyumba huyo ina bwawa kali la kuogelea, vyumba sita vya kulala na gym.
Crouch amekiri kuwa anapenda sana magari lakini amekuwa na wakati mgumu wa kupata gari la saizi yake.
Alidai kuwa hali hiyo inachangiwa na urefu wake wa futi 6 na inchi 7.
Alisema kutokana na hali hiyo, anakosa uhondo wa kuendesha magari makali na kufanya awe na magari ya kawaida tu.
Pamoja na changamoto hiyo, anamiliki magari aina ya Hyundai Santa Fe SUV, Aston Martin, Range Rover na Bentley.



Crouch alizaliwa katika eneo la Macclesfield, Cheshire lakini familia yake ilihamia Singapore alipokuwa na umri wa mwaka mmoja.
Walikaa huko kwa miaka mitatu na kurejea katika eneo la Ealing, London.
Akiwa na umri wa miaka 10, alipata nafasi ya kuwa muokota mipira katika uwanja wa Stamford Bridge.
Kutokana na urefu wake, Crouch ana majina mengi ya utani kama Crouchy, RoboCrouch, Crouchinho na Mr. Roboto.


Katika enzi yake akichezea Liverpool, mashabiki wa timu hiyo walikuwa wakimuimba "Crouch ni mrefu, anavaa jezi nyekundu na miguu yake haitoshi kitandani."
Jina la 'Mr Roboto' alipachikwa na mashabiki baada ya kuifungia England kwenye mechi ya kirafiki dhidi ya Hungary, Mei 30, 2006.
Alicheza dansi kwa staili ya Robot na akarudia tena kwenye mechi dhidi ya Jamaica, Juni 3, 2006.
Hata hivyo, alisitisha staili hiyo na kusema angeicheza kama England ingetwaa Kombe la Dunia mwaka 2006.
Crouch ana mke anayeitwa Abigail Clancy na wana mtoto anayeitwa Sofia.