Sunday, October 2, 2011

Umri kikwazo cha Drogba Ulaya


Nyota wa Chelsea, Didier Drogba amewataka watu waache kuzungumza habari kuwa anataka kuondoka katika klabu hiyo kwa kuwa hafikirii kwenda popote.
Habari kwamba mchezaji huyo anataka kuhamia Ujerumani zilisambaa baada ya kuonekana akiwa katika tamasha la Oktoberfest Jumapili iliyopita huko Ujerumani.
Drogba alikwenda katika tamasha hilo akiwa na lengo la kuchangia katika mfuko wa watoto lakini waandishi wa habari walilipoti kwamba hiyo ilikuwa ni hatua ya kuelekea Bayern Munich mwakani.
"Habari hizo ni uzushi mtupu, katika umri kama wangu si rahisi kuanza maisha mapya katika klabu nyingine."

Waafrika wanaokimbizana kwa utajiri Ulaya


Waliondoka barani afrika kwenda Ulaya kutafuta utajiri wa pesa. Sasa wanashindana kuvuna fedha katika klabu mbalimbali kubwa barani Ulaya. Wafuatao ni wanasoka watano wa Afrika wanaoongoza kwa utajiri katika soka la Ulaya.

Samuel Etoo (Dola 40 milioni)

KABLA hajapata mkataba mnono akiwa na klabu ya Anzhi Makhchkahala ya Russia, Etoío ndiye baba wa fedha miongoni mwa wachezaji wa Afrika wakiwa huko ng'ambo.
Etoío anakadiriwa kuwa na utajiri wa Dola 40 milioni. Kwa mwaka anaingiza kiasi cha Pauni 7 milioni. Hii ilikuwa wakati akiichezea Inter Milan kabla hajasaini mkataba mpya nchini Russia ambao unamlipa mara tatu ya kiasi hicho.
Kwa mwaka jana tu, Etoío aliingiza kiasi cha Dola 15 milioni kutokana na mikataba yake ya kibiashara na Puma na Ford pamoja na mshahara wake akiwa na Inter Milan. Kwa sasa ndiye mwanasoka anayelipwa zaidi duniani akipokea kiasi cha Pauni 365,000 kwa wiki akiwa amewaacha mbali mastaa kama Cristiano Ronaldo, Lionel Messi, Carlos Tevez, Kun Aguero na wengineo.
Aliwahi kuwanunulia wachezaji, makocha na maofisa wa timu ya taifa ya Cameroon kila mmoja saa yenye thamani ya Pauni 26,000 baada ya timu hiyo kufuzu kucheza fainali za Kombe la Dunia za mwaka jana. Etoío pia huwa hachukui pesa zozote za posho anaporudi kuichezea timu ya taifa huku akijikatia mwenyewe tiketi za ndege tofauti na wachezaji wengine.

Didier Drogba (Dola 30.7 milioni)

Kwa mujibu wa gazeti la Sunday Times, Drogba ana utajiri unaokadiriwa kufikia kiasi cha Pauni 19 milioni ambazo ni sawa na Dola 30 milioni akishika nafasi ya pili nyuma ya Etoío kwa wanasoka wa Kiafrika wanaotesa Ulaya.
Kwa mshahara wa mwaka, Drogba anaingiza kiasi cha Pauni 5.5 milioni huku akiwa na mkataba unaompatia kiasi cha Pauni 105,000 kwa wiki Stamford Bridge. Drogba ana mkataba mnono na kampuni ya vinywaji baridi ya Pepsi, lakini pia ana mikataba na kampuni za Nike na Orange France.
Kudhihirisha utajiri wake, mwishoni mwa mwaka 2009, Drogba alitoa kiasi cha Pauni 3 milioni kwa ajili ya ujenzi wa hospitali katika jiji la Abidjan nchini Ivory Coast.

Michael Essien (Dola 22 milioni)


Kwa mujibu wa gazeti la Sunday Times, kiungo huyu wa kimataifa wa Ghana anakadiriwa kuwa na utajiri unaofikia Dola 22 milioni ambazo ni sawa na Pauni 14 milioni.
Misimu miwili iliyopita, Chelsea ilimuongezea mshahara wake mpaka kufikia Pauni 80,000 kwa wiki na hilo liliongeza akaunti yake kwa kiasi kikubwa kwa mujibu wa takwimu zilizofanyika Mei mwaka huu.
Dosari kubwa katika utajiri wa Essien ni kitendo kilichoripotiwa miaka ya karibuni kuwa alikuwa amemtelekeza baba yake mzazi nchini Ghana bila ya kumjali kwa kile kinachoitwa tofauti za kifamilia. Hata hivyo kwa sasa wana maelewano mazuri na amemjengea nyumba ya kuishi.

Yaya Toure (Dola 11 milioni)

Mashine hii ya Manchester City inakadiriwa kuwa na utajiri wa Dola 11 milioni ambazo kwa pesa za Kiingereza ni sawa na Pauni 7 milioni. Yaya ni mmoja kati ya wachezaji wanaolipwa fedha nyingi duniani huku mkataba wake na Man City ukimpatia kiasi cha pauni 200,000 kwa wiki.
Mapato yake kwa mwaka yanakadiriwa kufikia Pauni 8.8 milioni lakini ataingiza Pauni 4 milioni na zaidi baada ya kukatwa kodi na serikali ya Uingereza. Hata hivyo, hapa amejumlishiwa na kiasi cha fedha alizokuwa anapata akiwa na Barcelona ya Hispania.
Baada ya kuipatia Manchester City nafasi ya kucheza katika Ligi ya Mabingwa Ulaya, Toure alipata kiasi cha Pauni 800,000 kama bonasi kwa mujibu wa mkataba wake na matajiri hao wa Man City.
Pamoja na utajiri wake, Yaya hapendi maisha ya anasa na hivi karibuni aliripotiwa akiwalaumu wanasoka wengi maarufu, hasa wa Ligi Kuu England kwa kuendekeza zaidi anasa mpaka asubuhi.

Kolo Toure (Dola 11 milioni)

Kaka wa Yaya Toure ambaye kitita chake kinatoka sare na cha mdogo wake kwa sababu ghafla Yaya anavuna pesa nyingi kwa wakati mfupi wakati Kolo amevuna kwa muda mrefu tangu akiwa Arsenal.
Kolo anapokea kiasi cha Pauni 120,000 kwa wiki akiwa na Man City huku mdogo wake akipokea Pauni 200,000 kwa wiki. Kwa mwaka Kolo anaingiza kiasi cha Pauni 5.7 milioni huku akijivunia pia mkataba wake na kampuni ya Adidas.
Kolo amejikuta katika wakati mgumu baada ya kufungiwa na FA ya England kwa kufeli vipimo vya kutumia dawa za kuongeza nguvu, lakini amerudi tena uwanjani Septemba baada ya kumaliza adhabu yake ya miezi sita.

Melissa Etheridge awakawaka


MSHINDI wa tuzo za Grammy na Oscar Melissa Etheridge ambaye anasumbuliwa na kansa ya matiti alikuwa kivutio katika tamasha la Hollywood Walk of Fame lililofanyika Jumanne ya wiki hii.
Sherehe hizo zilizofanyika Hard Rock Cafe huko Hollywood zilikuwa na nia ya kuzindua kampeni ya kukusanya fedha kwa ajili ya matibabu ya wanawake wenye kansa ya matiti kote duniani na Melissa alikuwa mtu wa mfano.
Melissa mwenye umri wa miaka 50, anajulikana kutokana na nyimbo zake za 'Come to My Window' na 'I'm the Only One.'
Mwanamke huyo ambaye aligundulika kuwa na kansa ya matiti mwaka 2004, amekuwa balozi wa kampeni dhidi ya kansa kwa miaka sita.

Lil Wayne ajivunia ukubwa


Rapa na mwimbaji nyota kutoka nchini Marekani, Lil Wayne wiki hii alitimiza miaka 29 na kutangaza kuwa ni miaka yake ya mafanikio katika maisha yake na kwamba anajivunia kuwatoa wanamuziki kadhaa akiwamo Nikki Minaj.
Lil Wayne ambaye ni baba wa watoto wanne, aliandika ujumbe huo kupitia akaunti yake ya Twitter na kusisitiza kuwa ataendelea kufanya kazi ya muziki daima kwani ndio kitu alichochagua.
Rapa huyo alianza kazi ya muziki akiwa na umri wa miaka 11, wakati huo alifanya kazi na rapa B.G mwaka 1997, akiwa na umri wa miaka 15, Wayne alijiunga na B.G. Kundi hilo lilifanikiwa baadaye mwaka 1999.
Wayne ambaye kwa sasa ameshatoa albamu tisa anasifika kwa kuwa na wapenzi wengi huku akiwa na kesi mbalimbali ambazo zimewahi kumfikisha mbele ya sheria.

Jennifer Hudson kufungua gym


Mwanamuzi na mwigizaji nyota Jennifer Hudson amesema anategemea kuonyesha dhamira ya kujenga maisha yenye afya njema kwa kufungua kituo cha mazoezi maalum ya kupunguza uzito mjini Chicago.
Jennifer ambaye anatokea katika mji wa Chicago atafungua kituo hicho Jumanne ijayo ambapo ameamua kukiita Jennifer Hudson Weight Watchers Center.
Meya wa Jiji la Chicago, Rahm Emanuel anatarajiwa kuhudhuria tukio hilo litakalofanyika katika kitongoji cha Hyde Park Kusini mwa Chicago.
Walinzi wa eneo hilo wamesema kuwa katika hafla hiyo kutakuwa na mchango wa heshima kwa ajili ya watu watatu waliokufa eneo hilo.

Lady Gaga akosa mvuto


Umaarufu wa mwanamuziki Lady Gaga unaanza kuporomoka baada ya kupata mikasa mbalimbali ya maisha huku suala la kujifanya mtu wa pekee likionekana kuwakera mashabiki. Mmiliki wa televisheni Simon Cowell wiki hii amemtaja Lady Gaga kuwa mwanamuziki anayewakera watu wengi duniani.
Mchambuzi huyo wa masuala ya muziki alisema kuwa Beyonce Knowles, Katy Perry ndio wasanii wa kike wanaofanya vizuri kwa sasa na wamekuwa wakiingia katika chati ya muziki ya Billboard mara kwa mara.
"Hawa ndio wanaoonekana mara kwa mara katika vyombo vya habari kwa sasa. Lady Gaga haonekani sana kwa sababu anawakera mashabiki, labda televisheni ndio zinajitahidi kummulika," alisema Cowell.
Simon Cowell aliendelea kumponda mwanamuziki huyo kwa kusema utafiti alioufanya amegundua kuwa Gaga ni mwanamuziki anayefahamika sana kutokana na kujitangaza kupitia mavazi.

Shakira apendelewa tuzo za Latin Grammy


Waandaaji wa tuzo za Latin Grammy wamemtaja mwanamuziki mkongwe wa nchini Colombia, Shakira kuwa msanii wa mwaka baada ya jina lake kutokea katika vipengele mbalimbali vya kuwania tuzo hizo zitakazofanyika Novemba mwaka huu.
Shakira, ambaye amewahi kushinda mara tatu katika tuzo hizo atapewa tuzo ya heshima kwa sababu anakubalika katika jamii.
"Tunaona fahari kumpa heshima kubwa mwanamuziki huyu, ni mwanamke anayefanya kazi zinazowagusa wengi duniani yaani katika muziki na jamii kwa jumla," alisema Rais wa Latin Recording Academy, Gabriel Abaroa.
Shakira 34, ambaye anatambulika duniani kwa kibao cha "Hips Don't Lie" alianza kuwa maarufu kama mwanamuziki na mwimbaji mapema mwaka 1990, ambapo aliimba nyimbo za Kilatini na muziki wa Mediterania

Mourinho awafukuza kazi makocha Inter Milan


Pamoja na kwamba bado hajapata ubingwa Ligi Kuu Hispania tangu alipojiunga na Real Madrid Mei 31, 2010, Jose Mourinho bado ni mmoja wa makocha wenye vipaji vya hali ya juu duniani.
Alidhihirisha ubora wakati alipoipatia Inter Milan ubingwa wa Serie A, Coppa Italia na Ligi ya Mabingwa Ulaya mwaka 2010. Kitu cha kuchekesha ni kwamba miezi 15 tangu alipoondoka katika klabu hiyo tayari makocha watatu wameajiriwa na kutimuliwa. Kuna sababu kadhaa zilizosababisha hali hiyo, lakini sababu ya msingi ni makocha hao kushindwa kuchukua vema nafasi ya kocha Mourinho. Tayari Rafa Benitez, Leonardo na Gian Piero Gasperini wametimuliwa na juzi tu ameingia Claudio Ranieri.
Ranieri, alichukua kibarua wiki iliyopita baada ya kutimuliwa kwa Gian Piero Gasperini. Kwa kumbukumbu za haraka, mkanda kamili ulianza wakati mmiliki wa Chelsea Roman Abramovich alipompa kazi kocha ambaye alianza kama mtafsiri wa Bobby Robson wakati alipoiongoza Barcelona, Huyo si mwingine ni Jose Mourinho. Kocha huyo tayari alikuwa amepata mafanikio katika kikosi cha FC Porto. Alipata Kombe la Uefa, 2003 akifuatia na ubingwa wa Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu uliofuata ulimfanya awe amekusanya vikombe vyote muhimu akiwa nyumbani. Na baada ya hapo alitua England.
Baada ya mafanikio akiwa Chelsea kocha huyo alihamia Inter Milan alipata ubingwa wa Serie A, Ligi ya Mabingwa Ulaya mwaka 2010 kabla ya kuhamia Real Madrid, sasa anatafuta uwezekano wa kuimaliza Barcelona.
Jose alipendwa sana akiwa England hiyo ilitokana na ubora wake, alipata mafanikio ya kushangaza Italia na sasa anaendelea kusaka nafasi nzuri Hispania, wakati Mourinho akiwa na mafanikio hayo, Ranieri alikuwa Valencia ambapo baadaye aliacha kazi na kutua Parma, kisha Juventus na kumalizia Roma. Sasa kocha huyo anataka kufanya kazi ya Mourinho iliyowashinda makocha wengine.
Si vizuri kumtabiria haraka kocha huyo, lakini historia inaonyesha kwamba kama akishindwa kufikia mafanikio kama ya Mourinho anaweza kutimuliwa mapema. Makocha wa awali waliondokaje?

Rafael Benitez

Huyu alikuwa kocha wa kwanza kuchukua nafasi ya Jose Mourinho katika kikosi hicho. Alipewa kazi baada ya kutimuliwa Liverpool ambapo licha ya kwamba kikosi kilikosa uelekeo, timu ilikuwa na historia ya kupata ushindi siku za nyuma na iliwahi kupata ubingwa wa Ligi ya Mabingwa Ulaya chini ya kocha huyo.
Kocha huyo aliendelea na nuksi alizotoka nazo Liverpool na viongozi wa ngazi za juu hawakuona ubunifu kutoka kwa kocha huyo na matokeo yake wakamtimua. Kilichomgharimu kocha huyo ni kushindwa kuendeleza pale alipoacha Mourinho. Ilikuwa ni majira ya Krismasi wakati mashabiki walipofahamu kuwa kocha mpya anatafutwa, lakini kitu kilichowashitua zaidi ni kuwa muhusika mwenyewe alikuwa ni mchezaji mkongwe wa wapinzani wao AC Milan, Leonardo.

Leonardo

Hakuwa mgeni San Siro, alifahamika zaidi kwa kuvaa jezi ya mistari ya rangi nyekundu na nyeusi siku za nyuma. Kocha huyo alianza vizuri lakini pia alijikuta ana kazi kubwa ya kufanya kabla ya kufikia mafanikio yaliyopatikana wakati wa Mourinho.
Inter ilijikuta ikiwa na wakati mgumu wa kuizuia AC Milan isipate Scudetto. Kitu kilichowachefua viongozi wa Inter Milan ni wakati Schalke 04 ilipoangusha mvua ya mabao 5-2 katika robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya na kuwavua ubingwa mabingwa hao watetezi. Kocha huyo ambaye awali alikuwa amesaini mkataba wa miezi 18 hakuwa na jipya na aling'olewa. Huyo naye aliondoka kwa sababu ile ile, alishindwa kuvaa vizuri viatu vya Mourinho.

Gian Piero Gasperini

Kocha mwingine alisakwa, awali uongozi ulitaka kumpa kazi Fabio Capello wa England lakini kocha huyo hakutaka na baadaye Gian Piero Gasperini akatupiwa mfupa uliomshinda fisi. Huyo naye aliingia katika historia ya Inter Milan ambapo ni kocha pekee aliyepewa kazi na kushindwa kupata ushindi katika mechi yoyote. Huyo hakuchukua muda mrefu, alitimuliwa wiki iliyopita.

Friday, September 30, 2011

Kweli Mwananchi linaongoza!!

Rais wa Zambia akisoma gazeti la Mwananchi siku moja baada ya kuapishwa, lililokuwa na kichwa cha habari Wapinzani wachukua Ikulu Zambia

Tuesday, September 27, 2011

Hatimaye mdogo wetu aenda India kwa matibabu

Mgonjwa anayesumbiliwa na matatizo ya moyo kwa zaidi ya miaka 11 , Sesilia Edward (katikati) akisindikizwa na Muuguzi wa Hospitali ya Regency, Mary Gomes (kushoto) na Dk Christopher Lucas, muda mfupi kabla ya kuondoka kwenda india kwa matibabu.

Lazima kieleweke!

Mkazi wa Manispaa ya Morogoro akiwa amebeba kiroba cha unga kichwani huku akiwa amepakiza kingine kwenye usukani wa baiskeli, eneo la Kituo cha daladala ziendazo nje ya manispaa hiyo.

Igunga bado, hebu tuombe mambo yaende vizuri Inshaallah

Waumini wa madhehebu ya dini ya Kikristo wakiwa kwenye maombi maalum ya kuombea Uchaguzi mdogo wa Jimbo la Igunga unatalajiwa Jumapili hii kufanyika kwa amani na utulivu, maombi hayo yalifanyika kwenye uwanja wa Sokoine mjini Igunga juzi jioni.

Ajali haina kinga, IGP chupu chupu

Mkuu wa Jeshi la Polisi, IGP Said Mwema (kulia) akifalijiwa na msamaria mwema baada ya kunusurika katika ajali ya gari iliyotokea juzi katika Barabara ya Kivukoni Front, mbele ya Ofisi za Takwimu na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa. Gari ya IGP iliyokuwa ikitokea Magogoni iligongana na gari ndogo.

Malori saba ya sukari yakamatwa Tarime

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tarime/Rorya, Deusdedit Kato (kushoto), akiwa na maofisa wa jeshi hilo mbele ya magari yaliyokamatwa kwa madai ya kukutwa yamebeba sukari kupeleka kuuzwa nchini Kenya.

Polisi Mkoa wa Tarime/ Rorya wamekamata malori saba ya sukari yaliyobeba tani 93.70, kutokana na operesheni ya kupambana na magendo iliyoshamiri ya uvushaji sukari kwenda Kenya.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tarime/Rorya, Deusdedit Kato, alisema walikamata mifuko 49 yenye ujazo wa kilo 50 kila mmoja nyumbani kwa mkazi wa Sirari. Alisema tani 2.45 zilitoka Tarime na tani 91.25 Musoma.

Kato alisema kwenye ukamataji walibaini mbinu ya kuhamisha sukari kutoka kwenye mifuko yake ya asili na kuwekwa mifuko mingine, ambayo ilikamatwa ikiwa tupu ya Kampuni ya Sukari Kilombero, huku sukari ikiwa imeondolewa.

Alisema sukari hiyo ilikuwa imejazwa upya kwenye mifuko ya South Nyanza Sugar ya Kenya na kwamba, shughuli hiyo hufanyika nchini na nje ya mpaka wa Tanzania, ili isafirishwe kwa urahisi kwenda Kenya.

Kato alisema maghala mengi yaliyopekuliwa hayakuwa na sukari, inasadikiwa yameficha bidhaa hiyo baada ya kutangazwa operesheni na kuongeza kuwa, imebainika sukari ya Tanzania huingizwa Kenya kwa ushirikiano wa wahalifu wengine kutoka Kenya.

“Kwa kushirikiana na vyombo vingine vya dola na taarifa za kiintelijensia, tumeendesha operesheni hii kwa kukagua maghala yote na kuwahoji wahusika. Pia, tumeongeza doria kwenye njia zote za panya na halali, tumekamata mifuko ya sukari mingine ni ya hapa Tarime na malori mengine yamekamatiwa Musoma wakidai kuwa walikuwa wanakuja kuuza Tarime," alisema

Monday, September 26, 2011

Wanawake kushiriki uchaguzi Saudia


Wanaume nchini Saudi Arabia kwa mara ya kwanza katika historia ya nchi hiyo wameruhusiwa kushiriki kwenye uchaguzi.

Mfalme wa Saudi Arabia ametoa agizo akiwaruhusu wanawake kushiriki kama wagombea kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa na Baraza la Ushauri.

Sheria za Saudi Arabia zinawazuia wanawake wa nchi hiyo kushiriki kwenye shughuli zozote za kisiasa na pia kuwa na simu za mkononi na vilevile leseni za kuendeshea magari.

Ukiukwaji huo wa haki za wanawake huko Saudia ni mkubwa kwani wanawake wa nchi hiyo hawaruhusiwi hata kuingia kwenye maeneo mengi ya umma bila ya kuwa na mawalii au wasimamizi wao wa kiume.


UN yaanza kuijadili Palestina



Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa jana limeanza kushauriana kuhusiana na ombi la Palestina kutaka uwanachama kamili wa umoja huo, ingawa kura kwa ajili ya ombi hilo haitarijiwi kufanyika mnamo majuma kadhaa yajayo.


Marekani imetishia kutumia kura yake ya turufu kupinga ombi hilo, ikisisitiza kuwa ni mazungumzo tu ya ana kwa ana kati ya Israel na Palestina ndiyo yatakayoweza kuzaliwa kwa taifa la wapalestina.

Pande nne zinazojihusisha na amani ya Mashariki ya kati, Umoja wa Mataifa, Umoja wa Ulaya, Marekani na Urusi zimekuwa katika juhudi za kutaka njia ya kuyafufua mazungumzo kati Israel na Palestina.


Bill Clinton amshambulia Netanyahu


Rais wa zamani wa Marekani, Bill Clinton, amesema Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu, ndiye aliyesababisha kukwama mwenendo wa amani ya Mashariki ya Kati.


Katika mazungumzo yake ya kidiplomasia pembezoni mwa kikao cha 66 cha Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, Clinton amesisitiza kuwa, Netanyahu ndiye anayebeba dhima ya kukabiliwa na mkwamo mwenendo wa amani ya Mashariki ya Kati.

Madai hayo ya Bill Clinton anayatoa katika hali ambayo, daima Marekani imekuwa ikiuunga mkono utawala wa wa Israel unaotenda jinai kila uchao dhidi ya wananchi wa Palestina.

Hayo yanajiri katika hali ambayo, Mahmoud Abbas Rais wa Mamlaka ya Ndani ya Palestina amewasilisha katika Umoja wa Mataifa ombi la Wapalestina la kutaka kutambuliwa nchi yao huru katika umoja huo, ambapo Marekani imetangaza wazi kwamba, itaupinga mpango huo na kwamba, itaupigia kura ya veto.


Prof Wangari Maathai afariki dunia



Mshindi wa tuzo ya amani ya Nobel kutoka Kenya, Profesa Wangari Maathai (Pichani), amefariki dunia hospitalini mjini Nairobi alikokuwa akitibiwa saratani.

Profesa Maathai, aliaga dunia juzi usiku hospitalini hapo alikokuwa anapewa matibabu.


Habari zinasema, Maathai, aliyeshinda tuzo hiyo mwaka 2004, alikuwa muasisi wa Shirika la Mazingira nchini Kenya.

Profesa Karanja Njoroge ambaye ni Mkurugenzi wa Green Belt Movement, shirika ambalo Prof Maathai alilianzisha amethibitisha kifo hicho.

Katika taarifa kwa vyombo vya habari Prof Njoroge alisema wakati wa kifo chake Wangari alikuwa na wanafamilia na marafiki.

Alisema Prof Maathai ambaye alikuwa na umri wa miaka 71, ameacha watoto watatu, wawili wakiume na mmoja wa kike.

Waasi wagundua kaburi lenye maiti 1,270 Tripoli

Ofisa wa Baraza la Mpito nchini Libya (Kulia), akiwaonyesha wapigapicha baki la sare ya gerezani ambayo imepatikana katika kaburi la pamoja la miili ya wafungwa zaidi ya 1,270 iliyogunduliwa na baraza hilo mjini Tripoli juzi. Mabaki hayo yanadhaniwa kuwa ya wafungwa waliouawa na maofisa wa usalama mwaka 1996 katika gereza la Abu Salim nchini humo.

Baraza la Mpito nchini Libya limesema kuwa, wameligundua kaburi la pamoja mjini Tripoli ambalo lina maiti 1,270.

Mabaki hayo yanadhaniwa kuwa ya wafungwa waliouawa na maofisa wa usalama mwaka wa 1996 katika gereza la Abu Salim.

Uasi dhidi ya Kanali Muammar Gaddafi ulianza kama maandamano kutaka wakili aliyewakilisha familia za wafungwa wa Abu Salim aachiliwe huru.

Uchimbuaji wa kaburi hilo la pamoja unatarajiwa kuanza hivi karibuni.

Msaada kwa mama


Watoto wakazi wa eneo la Nyang'andu kata ya Kivule Wilaya ya Ilala katika jiji la Dar es Salaam, wakielekea nyumbani kwao wakiwa wamebeba mboga za majani baada ya kutoka kununua.