Sunday, January 15, 2012

Mbunge Chadema afariki


Mbunge wa Viti Maalumu kwa tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Regia Estelatus Mtema (32), amefariki dunia baada ya gari alilokuwa akiendesha, kupinduka eneo la Mlandizi, Kibaha mkoani Pwani jana.

Ajali hiyo ilitokea saa 5:30 asubuhi karibu na Sekondari ya Ruvu, wakati mbunge huyo na watu wengine saba, wakisafiri kwa gari aina ya Toyota Landcruiser wakitoka Dar es Salaam kwenda Morogoro.

Akielezea mazingira ya ajali hiyo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Ernest Mangu, alisema mbunge huyo alifariki baada ya gari hilo alilokuwa akiendesha mwenyewe, kuacha njia na kupinduka.


Alisema ajali hiyo ilitokea baada ya Mtema kujaribu kulipita gari lililokuwa mbele yake na ghafla aliona gari lingine likija kasi mbele yake, katika kujaribu kulikwepa, ndipo gari hilo lilipinduka.

"Wakati akiwa hajalipita gari hilo aliliona gari lingine likija mbele kwa kasi , katika kulikwepa wasigongane uso kwa uso, alitoa gari lake barabarani na kusababisha kupinduka,’’ alisema Mangu.

Alisema watu wengine saba waliokuwa kwenye gari hilo walijeruhiwa, wawili kati yao hali zao zilikuwa mbaya, walipelekwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) Dar es Salaam kwa matibabu zaidi, huku wengine watano, wakiwahishwa Hospitali Teule ya Tumbi Kibaha.

Aliwataja majeruhi waliolazwa Tumbi kuwa ni Lawrence Mtokambali (58), Benadetha Mtema (50), Peter Madesa (50) na Rogers Abdallah(18).


Chadema yatoa tamko

Chadema kilisema kuwa Mtema alikuwa Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama hicho na Waziri Kivuli wa Kazi na alikuwa mchapa kazi hodari katika majukumu mbalimbali yakiwepo ya kijamii na kisiasa.

Taarifa hiyo iliyotolewa na Chadema jana na kusainiwa na Katibu Mwenezi wa chama hicho, John Mnyika ilieleza kuwa viongozi wakuu wa chama hicho wakiongozwa na Mwenyekiti wao Freeman Mbowe, Katibu Mkuu, Dk Willibroad Slaa, wajumbe wa Kamati Kuu, Wakurugenzi wa chama hicho makao makuu na wabunge, wameshtushwa na kifo hicho na kuungana na familia ya marehemu katika kipindi hiki kigumu cha majonzi.

Chadema kimesema taarifa zaidi kuhusu taratibu za maziko, itatolewa mara baada ya kukamilisha majadiliano kati familia ya marehemu, chama na Ofisi ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Kufuatia kifo hicho, mkutano wa Chadema uliokuwa umepangwa kufanyika jana Mjini Kibaha umehirishwa hadi itakapotangazwa wakati mwingine.



Elimu yake

Mtema alizaliwa Aprili 21, 1980. Alisoma elimu ya msingi kati ya mwaka 1989 na 1995. Alijiunga na Shule ya Sekondari Forodhani, Dar es Salaam mwaka 1996 hadi 1999 na kuhitimu kidato cha nne.

Aliendelea kidato cha tano 2002 na sita kati ya mwaka 2000 na 2002 katika Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Machame, mkoani Kilimanjaro.

Mwaka 2003 hadi 2006 alisoma Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUA) na kupata Shahada ya Maarifa ya nyumbani na Lishe.

Baada ya kuhitimu shahada yake, marehemu Mtema alifanya kazi katika taasisi mbalimbali kabla ya kujiunga na Chadema na kuteuliwa kuwa Ofisa Mwandamizi katika Kurugenzi ya Vijana ya chama hicho.

Baadaye aliteuliwa kuwa Ofisa Mwandamizi katika Kurugenzi ya Mafunzo ya chama hicho, nafasi ambayo aliishikilia hadi mwaka 2010 alipoteuliwa kuwa Mbunge wa Viti Maalum.


JK amtumia rambirambi Mbowe

Wakati huo huo, Rais Jakaya Kikwete amemtumia salamu za rambirambi Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe kufuatia kifo cha mbunge huyo.

Katika salamu hizo, Rais ameelezea kusikitishwa kwake na taarifa za kifo cha mbunge huyo na kueleza kwamba, marehemu Mtema amepoteza maisha akiwa kijana na kwamba pigo hilo si kwa Chadema pekee bali kwa taifa zima.

“Nimepokea kwa masikitiko na huzuni nyingi habari za kifo cha Mheshimiwa Mtema katika ajali ya gari. Siyo kwamba ajali hii imechukua maisha ya kijana bali imelinyang’anya taifa mbunge hodari, na kwa hakika, kifo chake siyo tu ni pigo kwa chama chako bali ni pigo kwa sote na kwa taifa letu kwa jumla.

"Nakutumia wewe binafsi, chama chako na wanachama wake salamu za dhati ya moyo wangu kuomboleza kifo na msiba huu mkubwa," alisema Rais Kikwete kupitia taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu.

Aliongeza: “Napenda ujue kuwa niko nanyi katika msiba huu. Napenda vilevile uniwasilishie salamu zangu za rambirambi za dhati kabisa kwa wana-familia, ndugu na jamaa wa marehemu Mheshimiwa Mtema.

Taarifa hiyo imemwomba Mbowe kufikisha salamu za Rais Kikwete kwa familia ya mbunge huyo na kuijulisha kuwa amepokea habari hizo kwa huzuni kubwa.

"Wajulishe kuwa nawaombea kwa Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema, awajalie uvumilivu na subira katika kipindi hiki kigumu kwa sababu yote ni mapenzi yake.





Ajali ya meli, Watu 70 wapotea, nahodha wa meli akamatwa


Wakuu wa forodha nchini Italia wamesema watu 70 wamepotea, baada ya meli ya abiria iliyobeba watu zaidi ya 4000 kwenda mrama katika mwambao katika Visiwa vya Tuscany nchini humo.

Meli hiyo ya abiria iitwayo Costa Concordia iligonga mwamba baharini na kusababisha tundu la mita 70 hadi 100 katika eneo lake la mbele, muda mfupi baada ya kuanza safari yake Ijumaa kutoka bandari ya Civitavecchia karibu na mji wa Roma.


Kikosi cha majanga kikiingia katika meli hiyo kuokoa abiria

Zaidi ya watu 42 wamejeruhiwa, ambao watu watatu hali zao ni mbaya na wengine 70 ambao ni miongoni mwa watu waliokuwa ndani ya meli hiyo hawajulikani walipo.

Meli hiyo ambayo ilikuwa imebeba abiria na wafanyakazi wapatao 4,000 ilipinduka upande mmoja. Hata hivyo, waokoaji nchini humo wanaendelea na juhudi za kutafuta watu waliopotea, baada ya meli hiyo ya abiria kupinduka.

Manrino Giampedron (57), mtumishi wa meli hiyo naye alikuwa miongoni mwa walionusurika, yeye alikuwa wa tatu kuokolewa na inasadikiwa alivunjika mguu wake mmoja

Mkuu wa kazi za uokoaji alisema hawawezi kuthibitisha idadi ya watu waliopotea kutokana na hali ya taharuki iliyopo iliyosababishwa na ajali hiyo. Hata hivyo, wakuu wa forodha nchini humo wanakadiria watu 70 wamepotea.

Habari zinasema kuwa, abiria mmoja alisema kuwa walikua wajitayarisha kwa chakula cha usiku waliposikia kishindo kikubwa kabla ya meli hiyo, kutikisika na kusimama na taa kuzimika.













Kile kibox (black box) kilipatikana, hiki ndicho kitakachotoa uhakika wa kujua ajali hiyo ilisababishwa na nini

Hii ni sehemu ya chini ya meli inavyoonekana ilivyoharibika baada ya kugonga mwamba huo, hapa linaonekana jiwe likiwa bado limeng'ang'ania sehemu hiyo hata baada ya kuitoboa.

Hapa anaonekana raia akishangaa

Uokoaji ulikuwa wa hali ya juu, hapa waokoaji walitumia helkopta pia

Nahodha akamatwa

Wakati huohuo, vyombo vya habari nchini humo jana vimeripoti kuwa nahodha wa meli hiyo, amekamatwa wakati uchunguzi unafanyika juu ya madai ya kuua bila kukusudia na kuitelekeza meli yake.

Nahodha wa meli hiyo, Francesco Schettino akiwa mikononi mwa polisi

Mkuu wa kampuni inayomiliki meli hiyo, Gianni Onorato, alisema ushahidi wa awali unaonyesha kuwa meli iligonga mwamba kisha nahodha kwa haraka akafuata utaratibu wa kuwatoa abiria melini.


Friday, January 6, 2012

Twende tukaone maajabu Rubondo


Ninashawishika kuwaalika watanzania wenzangu kwamba twendeni tukaone maajabu katika hifadhi inayoundwa na visiwa 11. Hii ni nyingine bali ni hifadhi ya Rubondo iliyopo wilaya ya Geita Mkoani Mwanza, ikiundwa na visiwa ambavyo ni

makazi ya ndege na wanyama wa aina mbalimbali.

Kwa namna vinavyoonekana, Rubondo ambayo iliyoanzishwa Januari 1977, inafananishwa na lulu ya kijani ndani ya ziwa Viktoria.

Inafikika kwa boti kupitia kituo cha Nkome wilayani Geita au Muganza upande wa wilaya ya Chato mkoani Kagera.

Awali kisiwa kilikaliwa na jamii ya Wazinza na kumbukumbu ipo eneo la 'Maji Matakatifu' yaliyotumika kwa tambiko la kupata baraka za miungu na samaki walipendelea eneo hili kuliko sehemu nyingine.


Wapo wanyama wa asili na baadhi hawapatikani katika hifadhi nyingine kama aina ya nzohe'statunga' huku hifadhi ikiwa na historia ya kuwa na uoto wa asili mithili ya misitu ya Kongo.


Moja ya matukio ya kushangaza ni ufundi wa baadhi ya wanyama ambao huogelea mpaka visiwa vingine vya hifadhi na baadhi hugeuka chakula cha wanyama wengine waishio majini.

Mkuu wa hifadhi Herman Batiho anasema mbali na kujivunia hazina ya wanyama kama tembo, twiga, viboko na mbega pia ni sehemu pekee unapoweza kuwaona kasuku wa kijivu kutoka Afrika Magharibi.

Ni eneo pekee ndani ya ziwa Viktoria linalotunzwa kwa ajili ya mazalia ya samaki.

Changamoto za kimazingira zinaongeza umuhimu wa sehemu hii kwa ajili ya maendeleo ya kiuchumi yanayotegemea rasilimali za ziwa.


Kubadilika kwa ubora wa maji ni dalili ya kubadilika kwa ikolojia ya ziwa ambapo matokeo ya Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi (Tafiri) mwaka 2009 sangara walipungua kutoka tani 750,000 mwaka 2006 hadi 227,365 mwaka 2010.


Ujangili mkubwa sio wa vipusa vya faru na tembo kama hifadhi ya Serengeti bali uvuvi wa sangara na watoto wao.

Mkuu wa hifadhi hiyo anasema ulinzi umeimarishwa kwa ajili ya usalama wa viumbe waliopo.


Kuelekea Kisiwa cha ndege

Safari ya kukifikia kisiwa cha ndege inapitia visiwa kadhaa ambavyo vina kila aina ya vivutio ukiwemo mwamba mkubwa ambacho ni kituo maalumu kwa ajili ya malezi ya watoto wa mamba.

Mayai huanguliwa kisiwa jirani na watoto husafirishwa kinywani hadi kwenye mwamba kuwakinga na maadui.


Baadhi hufa wakati wa safari na wachache hulindwa dhidi ya ndege hadi hatua ya kujitegemea.

Kisiwa cha Chambuzi kinapambwa na maelfu ya ndege kutoka Mashariki ya mbali, Afrika na Ulaya ambao hukimbia usumbufu utokanao na shughuli za binadamu na msimu wa baridi kali.


Kwa mujibu wa Christina Kibwe, mtaalamu wa ikolojia katika hifadhi ya taifa ya kisiwa cha Rubondo ni eneo pekee unapoweza kuona aina zaidi ya 200 za ndege na maelfu ya viota vyao vilivyochimbwa ardhini.


Hata hivyo ni vigumu kumuona ndege aina ya domo kiatu ambaye yuko katika kundi la vivutio vinavyotoweka na hupendelea maeneo ya ardhi oevu, kando ya mito na mabwawa.


Domo ni aina ya ndege wanaojulikana kitaalamu kama ‘balaeniceps rex’ na yuko hatarini kutoweka baada ya makazi yake kuharibiwa. Chakula chake kikuu ni samaki aina ya kambale na kamongo ambao huwasubiri waibuke.

Mtafiti katika Idara ya Zuolojia na uhifadhi wa viumbepori Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Jasson John anakiri ndege huyo atapotea katika uso wa dunia kama hatua za kumnusuru hazitachuliwa sasa.

Anasema ni kivutio kikubwa na hapa nchini wanakadiriwa kubaki ndege 200 ambao inabidi walindwe kwa mujibu wa sheria za wanyamapori na kuwa wapo ndege kati ya 5,000 na 8,000 waliobaki duniani.


Utafiti wa Mradi wa Mazingira wa Rufiji wa mwaka 2003 unatetea maarifa ya kimila na kisayansi kulinda viumbe hai. Mathalani wakazi wa maeneo hayo waliamini nyama ya kiboko hailiwi kwani hurutubisha maziwa kwa kinyesi.

Maarifa ya kimila mbali na kuokoa vizazi vya wanyama wa asili kama ilivyo katika hifadhi ya Rubondo, pia yamesaidia kuhifadhi maelfu ya hekta za misitu iliyoaminika kuwa makazi ya mizimu wakiogopa kuikasirisha kwa kuchoma moto.


Uhusiano na vijiji jirani

Utulivu wa ziwa uliniwezesha kusafiri bila shida katika boti ndogo hadi kijiji cha Nyabugela baada ya siku tatu za kutembelea visiwa vilivyozunguka hifadhi ya taifa Rubondo.

Vijiji jirani mbali na kufaidika na utalii pia vinaweza kusaidia utekelezaji wa sheria namba 5 ya mwaka 2009 inayozuia usafirishaji wa wanyama hai na kufanikisha mipango ya kudhibiti wizi wa rasilimali ambapo sekta ya utalii inachangia asilimia 17.2 ya pato la taifa.

Thursday, January 5, 2012

Urefu unamnyima gari bomba



Peter Crouch ni mshambuliaji wa Stoke City na kikosi cha England.
Akiwa na urefu wa futi 6 na inchi 7 anaaminika kuwa mchezaji mrefu zaidi kwenye Ligi Kuu England.
Crouch, ambaye alizaliwa Januari 30, 1981, alianzia soka yake katika timu ya watoto wa Tottenham Hotspur.
Hakupata nafasi katika kikosi cha kwanza cha timu ile na mwaka 2000 aliondoka na kujiunga na timu nyingine za Ligi Kuu.

Alichezea timu za Portsmouth, Aston Villa, Southampton na Liverpool kabla ya kurejea Tottenham mwaka 2009.
Ana utajiri wa kiasi cha pauni 15 milioni (Sh. 36.4 bilioni) na jumba la thamani la pauni 5 milioni (Sh 12.1 bilioni) katika eneo la Cheshire jijini Manchester.
Alinunua jumba hilo kutoka kwa nyota wa Kriketi wa England, Andrew ìFreddieî Flintoff.
Nyumba huyo ina bwawa kali la kuogelea, vyumba sita vya kulala na gym.
Crouch amekiri kuwa anapenda sana magari lakini amekuwa na wakati mgumu wa kupata gari la saizi yake.
Alidai kuwa hali hiyo inachangiwa na urefu wake wa futi 6 na inchi 7.
Alisema kutokana na hali hiyo, anakosa uhondo wa kuendesha magari makali na kufanya awe na magari ya kawaida tu.
Pamoja na changamoto hiyo, anamiliki magari aina ya Hyundai Santa Fe SUV, Aston Martin, Range Rover na Bentley.



Crouch alizaliwa katika eneo la Macclesfield, Cheshire lakini familia yake ilihamia Singapore alipokuwa na umri wa mwaka mmoja.
Walikaa huko kwa miaka mitatu na kurejea katika eneo la Ealing, London.
Akiwa na umri wa miaka 10, alipata nafasi ya kuwa muokota mipira katika uwanja wa Stamford Bridge.
Kutokana na urefu wake, Crouch ana majina mengi ya utani kama Crouchy, RoboCrouch, Crouchinho na Mr. Roboto.


Katika enzi yake akichezea Liverpool, mashabiki wa timu hiyo walikuwa wakimuimba "Crouch ni mrefu, anavaa jezi nyekundu na miguu yake haitoshi kitandani."
Jina la 'Mr Roboto' alipachikwa na mashabiki baada ya kuifungia England kwenye mechi ya kirafiki dhidi ya Hungary, Mei 30, 2006.
Alicheza dansi kwa staili ya Robot na akarudia tena kwenye mechi dhidi ya Jamaica, Juni 3, 2006.
Hata hivyo, alisitisha staili hiyo na kusema angeicheza kama England ingetwaa Kombe la Dunia mwaka 2006.
Crouch ana mke anayeitwa Abigail Clancy na wana mtoto anayeitwa Sofia.

Kimenuka CUF, Hamad, wenzake watimuliwa


Hatimaye Mbunge wa Wawi, Hamad Rashid Mohamed na wenzake watatu wamefukuzwa uanachama wa CUF kuanzia jana. Hatua hiyo ilichukuliwa na zaidi ya robo tatu ya wajumbe wa Baraza Kuu la chama hicho katika kikao chake kilichofanyika hapa.

Uamuzi huo umekata mzizi wa fitina wa hatma ya Hamad na washirika wake hao kisiasa ndani ya chama hicho, baada ya kuibuka mvutano wa muda mrefu kati yake na uongozi wa juu.

Mvutano huo uliochomoza zaidi baada ya Hamad kutangaza kuwania nafasi ya Katibu Mkuu inayoshikiliwa na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharrif Hamad.

Hata hivyo, hatua hiyo imepingwa na Hamad ambaye ameiita kuwa ni ya kihuni kwani imekiuka amri ya Mahakama iliyotangaza kusitishwa kwa kikao kilichochukua uamuzi huo.

Naibu Katibu Mkuu wa CUF (Bara), Julius Mtatiro alithibitisha kuvuliwa uanachama kwa Hamad na kuwataja wengine walioondolewa pia kuwa ni Mjumbe wa Baraza Kuu (Tanga), Doyo Hassan Doyo, Mjumbe wa Baraza Kuu (Pemba), Shoka Khamis Juma, Mjumbe wa Baraza Kuu Unguja, Juma Saanane na Mjumbe wa Baraza Kuu (Mbeya), Yassin Mrotwa.

“Kwa mujibu wa katiba ya chama, wasioridhika na uamuzi huo wanaweza kukata rufaa kwenye mkutano mkuu wa taifa,” alisema.


Wanandoa waadhimisha miaka 75 ya ndoa


Kama kuna yeyote anayefahamu siri ya kudumu kwa ndoa, basi ni Robert and Susan Erskine.

Walizama katika penzi mara tu walipoonana. Wakati huo Susana akiwa na umri wa miaka 20 na mume wake Robert akiwa na umri wa miaka 21.

Penzi hilo lilichanua na kudumu mpaka leo hii katika sikukuu ya kusherehekea mwaka mpya wa 2012 wameadhimisha miaka 75 ya ndoa yao.

Robert, 100 na Susan 99 walifanya sherehe hiyo iliyojumuisha vizazi vyao vitatu. Yaani watoto, wajukuu na vitukuu vyao.

Wapenzi hawa, walifunga ndoa baada ya miaka mitano ya uchumba, mwaka 1937 na tangu vita vya ya pili dunia, hawakuwahi kutengana kwa zaidi ya siku moja.

Susan anasema walifunga ndoa yao siku ya mwaka mpya kwa sababu hapo zamani, ukikosa kuhudhuria kazi- hulipwi, na sisi tulitaka kila mtu ahudhurie ndoa yetu. Ndiyo maana tukafunga ndoa yetu siku ya mapumziko.

“Nampenda Robert sana sasa hivi kama ambayo nilimpenda siku ya kwanza nilipomuona kwa macho yangu. tulipokutana, tu tulijua kuwa tunapendana. Bado tunapigana busu na kushikana mikono,” anasema Susan.


Walikutana wapi?

Walikutana kijijini kwao Bo’ ness in Stirlingshire, katika kwaya ya kanisani.

Susan anasema mama yangu alimkubali Robert kwa sababu alimuona kuwa ni kijana mzuri ambaye hatumii pombe wala kuvuta sigara.

“Na mpaka leo hagusi hata tone la pombe,” anasema Susan.

Baada ya Robert kurudi kutoka katika vita kuu ya pili ya dunia, walihamia Edingburgh ambako alipata kazi nyingine na Susan.

Wanandoa hawa walirudi nchini Bo’ness miaka 25, baadaye na ndipo waliposherehekea maadhimisho yao ya ndoa, pamoja na watoto wao.

Susan na Robert wana watoto watatu, William, 68, Margaret, 64 na Bobby 54. Wana wajukuu sita na vitukuu sita.

Susan anazungumzia namna ambavyo ndoa nyingi katika ulimwengu wa sasa zinavyovunjika na kusema, mapenzi mengi siku hizi si ya kweli.

Anaongeza na kusema unapoingia katika ndoa unatakiwa ujipange.

“Uwe kama mwanamke halisi, usijifanye mwanaume, kwa mfano mimi nafanya kazi zote za ndani, wakati Robert anafanya kazi ndogondogo kama kutupa taka na kupanda maua,” anasema Susan.

Anaendelea na kusema kuwa pamoja na kupendana sana, lakini wana tabia tofauti. Wakati Susan ni mzingumzaji na anayependa kucheka, Robert ni mkimya.


“Napenda utani, yeye ni mkimya, anapenda kuniambia kuwa, ninaongea sana kwa hiyo hapati nafasi ya kuongeza neno,” anasema Susan.

Anasema ili ndoa zidumu ni vyema kila mmoja akatambua udhaifu wa mwenzake na ahakikishe anaulewa na kuukabili.

Wakati Susan na Robert wanasherehekea miaka 75 ya ndoa, zipo ndoa ambazo zimedumu kwa saa chache tu. Na watu hao ni mwanamuziki Britney Spear na Jason Alexander ambao ndoa yao ilidumu kwa saa 55 tu.

Tuesday, January 3, 2012

Baba kapata mama, mama kapata baba

Picha linaanza, hapa ndio mzee ninamalizia utaratibu wa kuchukua jiko
Baada ya ndoa tukapiga picha


Siku ya pili mke wangu akaenda Salon kupambwa tayari kwa Reception, alipambwa na wale wajuaji wa mjini, Twaiba Classic salon




Mambo ya Twaiba hayo, si kupamba tu...hayta pamba unapata hapa

Hii ni copy ya kipeperushi nilichowatengenezea

Baadaye tukaingia Ukumbini, Banora pale jirani na Mlimani City
Tuliwakaaaaaaaaaaaaaa!!!!
Vyengine tulipata maelekezo toka kwa waliotutanguli, huyu ni dada yangu jamani
Tukajichana, weweee!! We acha tu!!
Pia tukapewa vilivyo vyetu, walivyotuandalia kututunza



Tulijazwa na mijihela vilevile
Mama yangu (kushoto) na mama mkwe wangu
Baba yangu (kushoto) na baba mkwe wangu
Baba mkwe akimchum mwanaye

Hii ndiyo familia yetu
Pongezi kibaoooo
Mmeionaaaa!!



Baba na mama mkwe


Tukajimwaga mpaka mwishoooooooooo!!!