Sunday, July 8, 2012
Sunday, July 1, 2012
Hivi mnapata wapi leseni?!..
Thursday, June 28, 2012
Huu ni UNYAMA
NI unyama. Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari Tanzania, Dk Steven Ulimboka ametekwa na watu wasiojulikana, kupigwa na kujeruhiwa sehemu mbalimbali za mwili, kisha kutupwa katika Msitu wa Pande, nje kidogo ya jiji Dar es Salaam.
Daktari huyo ambaye amekuwa akiratibu mgomo wa madaktari unaoendelea, aliokotwa na msamaria mwema akiwa amefungwa mikono na miguu akiwa katika hali mbaya.
Baada ya kuokotwa na wasamaria wema na kufikishwa katika Kituo cha Polisi, Dk Ulimboka aliwahishwa katika Taasisi ya Mifupa Muhimbili (Moi) kwa matibabu, na ilielezwa kuwa hali yake haikuwa nzuri.
Taarifa za kujeruhiwa kwa Dk Ulimboka zilisambaa kwa kasi katika vyombo vya habari, mitandao ya kijamii na ujumbe mfupi wa simu.
![]() |
| Gari la wagonjwa lililokuwa limembeba Dk Steven Ulimboka likiingia katika hospitali ya Taifa ya Muhimbili jana huku likiwa limezongwa na Madaktari. |
Kutokana na tukio hilo, wanaharakati wa haki za binadamu wameituhumu Serikali kuhusika na tukio hilo, huku Serikali ikikana tuhuma hizo, na papohapo ikiagiza Jeshi la Polisi kuwasaka waliohusika.
Akisimulia mkasa huo kupitia Kituo cha Redio cha Clouds FM, Dk Ulimboka alisema tukio hilo lilitokea usiku wa kuamkia jana katika klabu ya Leaders jijini Dar es Salaam, alikokuwa na wenzake wawili.
Alisema baada ya kukaa kwenye baa hiyo kwa muda, alianza kujisikia vibaya tofauti na siku zingine.
"Mara, katikati ya maongezi tukaona mtu anaongea na simu. Ghafla tukiwa tunasema tuagane, wakaja watu kama watano hivi na bunduki, wakasema wewe na yule bwana mko free (huru), tunakuchukua wewe (Dk. Ulimboka)," alieleza na kuongeza,
"Sijakaa sawa, nikaona nimeshaburutwa nikaanguka kwenye lami, wakaniinua na kuniingiza kwenye gari nyeusi, lakini ilikuwa haina namba."
![]() |
| Madaktari wakiwa wamebeba Dk Steven Ulimboka kumwamisha kutoka katika Chumba wagonjwa mahututi baada ya kupata huduma ya kwanza kutokana kupigwa na watu wasiojulikana. |
Taarifa zaidi kutoka Moi alikolazwa kwenye chumba cha uangalizi maalumu, zilieleza kuwa baada ya uchunguzi, ilibainika kuwa daktari huyo aliteswa vibaya, ikiwamo kuumizwa sehemu za siri, kuvunjwa meno kadhaa, mbavu na miguu.
Habari zaidi zilisema kuwa, baada ya kufikishwa katika Msitu wa Pande na kupata kipigo, alizimia kwa muda na alipozinduka aliwachomoka watekaji hao na kujaribu kukimbia.
Msitu wa Pande ulioko wilayani Kinondoni, ndiko wafanyabiashara watatu wa madini kutoka Mahenge, Morogoro na dereva teksi wa Manzese Dar es Salaam waliuawa na polisi mwaka 2006.
Chanzo chetu cha habari kilisema, baada ya Dk Ulimboka kujaribu kuwatoroka watekaji, walipiga risasi mbili hewani, aliposimama wakamshika na kumpa kipigo na mateso zaidi, hivyo kusababisha avunjike maeneo mbalimbali ya mwili.
Polisi waunda tume
Jeshi la Polisi limeunda jopo kuchunguza tukio la utekaji nyara na shambulio la kudhuru mwili wa Dk Ulimboka.
Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova alisema jana kuwa tukio hilo ni la aina yake na kwamba halijawahi kutokea hapa nchini.
Alisema jopo hilo ambalo linaongozwa na Kamishna Msaidizi wa Polisi, Ahmed Msangi linahusisha wapelelezi wa fani mbalimbali.
“Ni issue (jambo) ambayo imetokea bila kutegemea katika namna ambayo ina utata, hivyo kazi yetu ni kutegua utata huo,” alisema Kova na kuongeza:
“Hatutaki katika nchi yetu matukio kama haya yawe ya kawaida, tunataka liwe la mwanzo na la mwisho.”
Kamanda huyo alisema yeye alipata taarifa za kutekwa Dk Ulimboka usiku wa kuamkia jana saa 7 usiku.
Kwa mujibu wa Kamanda Kova, Dk Ulimboka aliokotwa na raia mwema katika eneo la Msitu wa Pande jana saa 2:30 asubuhi karibu na barabara huku akiwa na majeraha sehemu mbalimbali za mwili, ikiwamo kichwani na mikononi.
Alisema raia huyo (jina limehifadhiwa) alitoa taarifa katika Kituo cha Polisi Bunju, na askari walikwenda kwenye gari la raia huyo na kumkuta Dk Ulimboka wakamchukua na kwenda naye ndani.
Kova alisema: “Aliyemuokota alisema alimkuta amefungwa mikono na miguu, na inaonekana kama watu hao walikuwa wanalipiza kisasi.”
Kwa mujibu wa kamanda huyo, akiwa kituoni hapo, Dk Ulimboka alijieleza kwamba juzi saa 5:30 usiku akiwa katika klabu ya Leaders na wenzake wanapata vinywaji pamoja na wateja wengine, walikuja watu watano na kuwatishia.
Alisema watu hao waliwataka walale chini na kwamba walitii, kisha watu hao walimchukua Ulimboka na kuwaambia wengine waendelee na vinywaji.
“Ulimboka alisema watu hao walikuwa na gari aina ya Escudo lenye rangi nyeusi na hili gari halikuwa na namba na walichukua ufunguo wake wa gari, nyaraka kadhaa na hela alizokuwa nazo,” alisema Kova.
Alisema akiwa katika gari hilo na watu wengine watano, ghafla walianza kumpiga huku wakiwa hawasemi chochote na kwamba baadaye walimfunika kichwani na fulana nyeusi hadi Msitu wa Pande.
Kova alisema baada ya maelezo hayo, Dk Ulimboka alitoa namba za simu za rafiki yake Dk Deogratius, na baada ya hapo alipewa fomu ya matibabu (PF3) na kupelekwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) kwa matibabu.
Kamanda huyo alitoa wito kwa wananchi na mtu yeyote mwenye taarifa kamili kuhusu tukio hilo atoe taarifa, kwani lisipojulikana vizuri linaweza kuzua minong’ono mingi.
Askari ajeruhiwa MNH
Katika hatua nyingine, Kova alisema watu wasiojulikana wamemjeruhi Mkuu wa Upelelezi wa Kituo cha Polisi cha Selander Bridge ambaye alikwenda MNH kufanya upelelezi wa tukio hilo.
Kwa mujibu wa Kova, Mkuu huyo wa upelelezi alijeruhiwa wakati akiwa anaongea na simu, na kwamba watu hao pia walimpora vitu alivyokuwa navyo ikiwemo simu.
Mkurugenzi Moi
Mkurugenzi wa Tiba katika Taasisi ya Mifupa Muhimbili (Moi), Cuthbert Mchalo alisema majeruhi huyo alifikishwa hospitalini hapo saa 4:25 asubuhi, kwa msaada wa gari la wagonjwa la Kampuni AAR, kutoka Kituo Kidogo cha Polisi Bunju.
“Tumempokea, anaendelea vizuri na amepata maumivu katika maeneo ya kifuani, kichwani na tumboni,” alisema na kuongeza kuwa taarifa zaidi zitatolewa baadaye.
Alifafanua kwamba kwa sasa wanajitahidi kumpatia matibabu, ingawa alipelekwa hospitalini hapo akiwa katika hali ambayo siyo nzuri, na uchunguzi zaidi unaendelea.
Wanaharakati walaumu Serikali
Miongoni mwa watu wa kwanza kufika katika Kituo cha Polisi Bunju kumuona Dk Ulimboka ni Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk Hellen Kijo-Bisimba ambaye alisema kilichotokea kinaonyesha jinsi gani Serikali ilivyo na woga katika kushughulikia matatizo ya wananchi.
Dk Bisimba alisema wao wanaamini kuwa tukio hilo lina mkono wa Serikali na kama ni kinyume cha hapo, basi inapaswa kuwaridhisha wananchi kuwa hawana mkono wao katika sakata hilo.
“Kama wao hawana mkono wao basi wanapaswa kuwaridhisha wananchi kuwa hawahusiki kwa kuwatia mbaroni wahusika na kuwafikisha katika vyombo vya sheria,” alisema Bisimba.
Mkurugenzi huyo alisema matamshi ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda bungeni jana kuwa wanashughulikia suala la madaktari na watalimaliza liwalo na liwe inaleta tafsiri kuwa kilichotokea kina mkono wao.
“Alivyosema liwalo na liwe na kinachotokea sasa kinabainisha kuwa mengi zaidi yatafuata,” alisema Bisimba na kuongeza kuwa hali hiyo inasikitisha na haikuwahi kufikiriwa.
Bisimba alisema baada ya wasamaria kumkuta mnamo saa 12:00 asubuhi, walimpeleka katika kituo kidogo cha Polisi cha Bunju ambako polisi walifungua mashtaka ya wizi wa maungoni na kupatiwa RB yenye namba BJ/RB/1870/2012.
“Mimi nilipata taarifa za kutekwa kwake kutoka kwa mwenzie aliyekuwa naye mnamo saa nane usiku, na baada ya kupata taarifa hizo niliwaeleza wanaharakati wenzangu juu ya hatua za kuchukua,” alisema Bisimba.
Bisimba alisema aliwasili katika Kituo cha Polisi cha Bunju, jana mapema asubuhi na kumkuta Dk Ulimboka akiwa amejeruhiwa vibaya, lakini hakuwa amepatiwa huduma yoyote.
“Tulikwenda kumchukua na kukuta hali yake ni mbaya, lakini cha ajabu pamoja na majeraha yote hakupatiwa msaada wowote wa huduma, jambo ambalo lilitusikitisha sana,” alisema.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Sikika, Irenea Kiria alisema kilichotokea ni kitu kibaya na kinaonyesha jinsi gani Serikali inavyoshughulika na watu, badala ya kujali hoja za msingi ambazo zinawasilishwa.
Kiria alisema hoja za madaktari zilipaswa kusikilizwa kwani licha ya madai ya masilahi yao lakini pia wanapigania mazingira bora yenye utu kwa ajili ya wagonjwa.
Madai mengine ni upatikanaji wa dawa na vifaa tiba kwa ajili ya kuwahudumia wananchi pamoja na upatikanaji wa dawa, mambo ambayo alisema hayahitaji mjadala.
“Suala la masilahi ya madaktari linazungumzika lakini siyo suala la dawa, mazingira bora ya kuwahudumia wagonjwa na upatikanaji wa vifaa tiba na vipimo vingine,” alisema Kiria.
Nchimbi: Tutawasaka
Kwa upande wake Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk Emmanuel Nchimbi alisema Serikali imeliagiza Jeshi la Polisi kuwasaka na kuwachukulia hatua watakaobainika kuhusika na utekaji huo.
Dk Nchimbi alisema mjini Dodoma kuwa Serikali haihusiki kwa namna yoyote ile na utekaji nyara huo, na kwamba kitendo hicho kinapaswa kulaaniwa kwani hakikubaliki katika jamii hasa kwa zama hizi.
“Kwanza, madaktari ni watu muhimu ambao wao ndio wanaotuwezesha sisi kuishi, kwa hiyo wapo kwa ajili ya maisha yetu, hata kama asingekuwa daktari, kwa mtu yeyote yule, jambo hili halikubaliki katika nchi yetu,” alisema Dk Nchimbi na kuongeza:
“Tumewaagiza polisi wafanye uchunguzi ili kuwabaini wahusika na wakipatikana wafikishwe katika vyombo vya sheria, maana hatuwezi kwa namna yoyote kuvumilia vitendo vya aina hii.”
Alisema Serikali imestushwa sana na tukio hilo na haitavumilia kwa namna yoyote vitendo hivyo pamoja na vile vya unyanyasaji kwani ni kinyume cha sheria.
Kuhusu kupigwa kwa Mkuu wa Upelelezi (OC- CID), ASP Mukiri, Dk Nchimbi alisema lilikuwa ni tukio la bahati mbaya kwamba madaktari waliokuwapo Muhimbili walishindwa kuwa na uvumilivu kwani askari aliyepigwa alikuwa ameagizwa na Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kinondoni, Charles Kenyela kwenda kufuatilia matibabu ya Dk Ulimboka.
“Hapa ndipo ninapotofautiana na watu wengi, mnampigaje polisi, maana yule anapaswa kuwa rafiki wa raia, sasa unampigaje mtu ambaye ni mlinzi na umemwajiri, analipwa kwa kodi yako?” alihoji Dk Nchimbi.
Yaliyojiri bungeni
Tukio hilo lililosambaa kwa kasi katika mitandao ya kijamii na vyombo vya habari, liliibuka bungeni, ambako Mbunge wa Kawe (Chadema), Halima Mdee alilaani vikali kitendo cha watu wanaodaiwa ni maofisa wa vyombo vya usalama kumpiga Dk Ulimboka.
Alisema kitendo hicho ni unyama unaostahili kukemewa na kila mpenda amani hapa nchini.
“Tumestushwa na tukio hilo na tunalaani vikali kitendo hicho na kumwombea Dk Ulimboka ili apone haraka,” alisema Mdee.
Katika hatua nyingine, hospitali za Mwananyamala, Temeke na Amana, kujionea hali ilivyokuwa baada ya kusambaa kwa taarifa za kupigwa kwa Dk Ulimboka.
Katika hospitali ya Mwananyamala, wengi walioonekana walikuwa ni wauguzi huku madaktari wakidaiwa kwenda katika hospitali ya Muhimbili kumuona mwenzao aliyejeruhiwa.
Dk Ulimboka aliwahi kufanya kazi katika hospitali hiyo ya Mwananyamala katika miaka ya nyuma.
Hata hivyo, juhudi za waandishi kuzungumza na uongozi wa hospitali hiyo, hazikufanikiwa baada ya wafanyakazi wa Ofisi ya Mganga Mkuu kusema kuwa mganga huyo amekataa kuzungumza, akiwataka waandishi wafike ofisini kwake leo.
“Ameniambia niwapeleke kwa katibu wake, lakini na yeye nimemkosa, sasa nimerudi kwake ameniambia niwaambie mrudi kesho,” alisema katibu muhtasi wake.
Katika hospitali za Temeke na Amana, hali pia ilikuwa hivyo, baadhi ya wahudumu waliokutwa katika hospitali hizo wakikataa kuzungumza kwa madai kuwa wanaotakiwa kuzungumza hawapo.
Madaktari jeshini waitwa kazini
Monday, June 25, 2012
Lulu bado njia panda
SERIKALI imezidi kumweka katika wakati mgumu msanii wa filamu nchini, Elizabeth Michael ‘Lulu’, anayekabiliwa na kesi ya tuhuma za mauaji ya msanii mwenzake, Steven Kanumba.
Hatua hiyo inatokana na hatua ya upande wa mashitaka kukwamisha usikilizwaji wa kesi hiyo kwa kuwasilisha Mahakama ya Rufani maombi ya kupitiwa upya uamuzi wa Mahakama Kuu wa kukubali kufanya uchunguzi wa umri sahihi wa mshitakiwa huyo.
Umri wa Lulu umeibua utata wa kisheria baada ya upande wa utetezi kusema mteja wao ana miaka 17 na si 18 kama Hati ya Mashitaka inavyoonyesha, hivyo unadai kisheria anapaswa kushitakiwa katika Mahakama ya Watoto huku ule wa mashitaka ukipinga hoja hiyo.
Kufutia hali hiyo, mshitakiwa huyo aliyefika Mahakama Kuu jana Jumatatu kusikiliza shauri la utata huo wa umri wake, alishindwa kujizuia na kumwaga machozi baada ya mahakama hiyo kusimamisha shauri hilo.
Kufutia hali hiyo, mshitakiwa huyo aliyefika Mahakama Kuu jana Jumatatu kusikiliza shauri la utata huo wa umri wake, alishindwa kujizuia na kumwaga machozi baada ya mahakama hiyo kusimamisha shauri hilo.
Katika kesi yake ya msingi iliyoko Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Lulu anatuhumiwa kumuua Kanumba usiku wa Aprili 7, 2012 nyumbani kwa marehemu, Sinza, jijini Dar es Salaam.
Utata wa umri wa Lulu ulitarajiwa kusikilizwa hiyo jana Jumatatu na Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.
Juni 11, 2012 Mahakama Kuu iliamua kufanya uchunguzi wa usahihi wa umri wa msanii huyo kufuatia maombi yaliyowasilishwa mahakamani hapo na jopo la mawakili wanaomtetea.
Lakini jana Jumatatu, Wakili wa Serikali, Elizabeth Kaganda, asema mahakamani hapo kuwa upande wa Jamhuri tayari imewasilisha maombi Mahakama ya Rufani kuomba uamuzi huo wa Mahakama Kuu uliotolewana Jaji Dk. Fauz Twaib ufanyiwe marejeo.
Jaji Dk. Twaib alikubaliana na maombi haya Jamhuri na kusimamishwa usikilizwaji huo hadi Julai 9, 2012, ikiwa Mahakama ya Rufani itakuwa imemaliza kushughulikia maombi hayo ya Serikali.
Kabla ya mahakama kufikia uamuzi huo, mawakili wa Lulu, Kennedy Fungamtama na Peter Kibatala, walipinga maombi ya serikali wakidai ni mbinu ya kuchelewesha shauri hilo.
Fungamtama alidai kuwa hadi wakati huo mahakama ilipoanza hapa kuwa na amri yoyote ya Mahakama ya Rufani ya kusimamishwa usikilizwaji wa suala la utata wa umri wa mteja wao.
“Hata kwenye maombi haya hakuna maombi yanayoelekeza kusimamishwa kwa usikilizwaji wa maombi haya,” alisema Fungamtama.
“Kinachofanywa hapa ni matumizi mabaya ya mamlaka ya Ofisi ya DDP (Mkurugenzi wa Mashtaka).”
Kwa upande wake, Wakili Kibatala, alidai kuwa maombi hayo ya Jamhuri kwa Mahakama ya Rufani hayaoneshi mazingira ya kusimamishwa kwa usikilizwaji wa maombi hayo na kwamba hiyo inabaki kwa mamlaka ya Mahakama Kuu yenyewe.
“Lakini kwa maslahi ya mshtakiwa ambaye anaendelea kuteseka mahabusu, tunaiomba mahakama hii iamuru usikilizwaji wa maombi haya (utata wa umri ) uendelee,” alisisitiza Kibatala.
Lakini akijibu hoja hizo, Wakili Kaganda, alidai ofisi ya DPP inatambua matakwa ya haki na kwamba inatenda kwa matakwa ya haki haitumii vibaya mamlaka yake.
Lulu anaendelea kushikiliwa rumande kwa vile aina ya shitaka linalomkabili halina dhamana kisheria.
Thursday, June 21, 2012
Ajali iliyotokea leo Tegeta
Tuesday, June 19, 2012
Safari ya Drogba China yaiva
![]() |
| Add caption |
SHANGHAI, China
SAFARI ya mshambuliaji wa zamani wa Chelsea ya England, Didier Drogba kwenda kumalizia soka nchini China, imeiva na anatarajia kujiunga na timu ya Shanghai Shenhua wakati wowote wiki hii.
Nyota huyo wa kimataifa wa Ivory Coast ameelezwa kuingia mkataba wa miaka miwili wenye thamani ya pauni 25 milioni (sawa na Sh60.8 Bilioni).
Kwa sasa Drogba (34) yuko nchini India
Kwa mujibu wa bosi wa klabu hiyo ya China, Zhu Jun, Drogba anatarajia kutangaza uhamisho huo kwenye tovuti yake binafsi.
Mbali na timu hiyo ya China kumtaka drogba, klabu nyingine tajiri ya falme za Kiarabu, Al Wasl FC nayo imeonyesha nia.
safari yake ya China inatarajia kumkutanisha na mshambuliaji mwenzake aliyecheza naye pamoja kwenye kikosi cha Chelsea, Nicolas Anelka.
"Hatua inayofuata kwangu nimefurahi," alisema Drogba wakati wa ziara yake nchini India.
"Muda siyo mrefu nitatangaza uamuzi wangu, lakini kwa sasa ningependa msubiri kwanza," alisema Drogba.
Klabu hiyo ya China imekusudia kufanya mageuzi makubwa kwa kusajili wachezaji wengi wa kigeni pamoja na kocha pia.
Friday, June 15, 2012
Binti aliyehukumiwa kupigwa mawe hadi kufa kwa uzinzi
BLANKETI la uchungu na kukata tamaa limeufumbata uso wa Intisar Abdallah.
Ameketi katika chumba cha jela chenye joto kali, miguu yake ikiwa imefungwa kwa chuma,huku akiendelea kukinyonyesha kichanga chake chenye umri wa miezi mitano.
Intisar, ameathirika kisaikolojia kwa sababu anajua fika kuwa, siku si nyingi ataingizwa kaburini.
Machungu ya Intisar, (20) hayakomei katika hofu ya kifo pekee, bali hata namna na sababu ya kifo hicho.
Intisar, atachimbiwa ardhini na kubakizwa kichwa tu. Kisha atapigwa mawe hadi kufa ikiwa ni adhabu yake baada ya kuzini na kubeba mimba.
Aprili 22 mwaka huu ndiyo siku ambayo Hakimu, Sami Ibrahimu Shabo wa mahakama ya makosa ya jinai ya Ombada iliyoko katika mji mkuu wa Khartoum, Sudan alimhukumu Intisar adhabu kifo.
Kilimchofanya mpaka binti huyu akapewa adhabu hii ni kwa sababu alifanya tendo la ngono nje ya ndoa. Instisar ambaye ni mama wa watoto watatu alionekana mwenye kosa la jinai kwa nchi zenye misingi imara ya dini ya Kiislam.
Hukumu ya Intisar ilitolewa kwa sababu ya kifungu namba 146 cha mwaka 1991 cha makosa ya jinai nchini Sudan.
Awali, Intisar alishtakiwa kwa uzinzi, lakini akaachiwa huru. Baadaye, kaka yake alimpiga kikatili na kumshurutisha akimtaka akiri makosa yake.
Hapana shaka kipigo kile ndicho kilichomfaya Intisar akubali kosa hilo.
Hata hivyo, mwanamume waliyezini naye aliachiwa huru kwa sababu tu, alikana kosa hilo.
Wakati huo, kesi iliendeshwa kwa lugha ya kiarabu,ambayo Intisar haifahamu. Hukumu ikatolewa wakati Intisar akiwa hana wakili wa kumtetea katika hilo.
Mawakili waliruhusiwa kumwona na kumuhoji mara baada ya hukumu kutolewa.
Hukumu ya kuua haikubaliani na sheria za kimataifa, kwani inaenda kinyume na haki za binadamu.
Pamoja na hilo, lakini kibaya zaidi ni kumhukumu kifo mama mwenye mtoto mchanga ni kitendo kinachopingwa na sheria za kimataifa.
Hukumu hiyo ilipingwa vikali na mtandao wa kikundi cha Mapambano cha Wanawake waishio katika Pembe ya Dunia (SIHA network).
Siha kilitoa tamko kali kuhusu kesi hiyo na kusema imejaa upungufu, unyanyasaji na uvunjwaji wa haki kwa kiasi kikubwa.
“Ni ajabu kwamba mwanaume ambaye anatuhumiwa kuzini naye ameachiwa huru. Jambo ambalo linaweka wazi ukatili wa kijinsia na usimamizi mbaya wa migogoro ya kifamilia,” ulisema mtandao huo.
Sudan ya Kaskazini ni miongoni mwa nchi saba duniani zinazotoa adhabu ya kifo kwa kupigwa mawe.
Rais Omar Al Bashir ndiye aliyetambulisha chembechembe za Sharia Law, mwaka 1989 baada ya kuingia madarakani.
Lakini kinachowachanganya wengi ni kuwa, adhabu hizo huwapata zaidi wanawake kuliko wanaume.
Wananchi nchini humo wamekuwa wakifungwa vifungo vya muda mrefu na kupewa adhabu kali kwa makosa kama ya kuuza bidhaa barabarani, kuvaa mavazi yanayokwenda kinyume na taratibu za kidini pamoja uzururaji.
Watu wamewahi kupigwa mawe hadi kufa baada ya kufanya makosa ya uzinzi.
Julai 13, 1997 Changiz Rahimi alihukumiwa kupigwa mawe hadi kufa, huku akilipa faini kwa kuzini.
Julai 14, 1995 wanawake wawili Sada Abdali, 30, na Zeinab Heidary, 38 walihukumiwa kupigwa mawe katika Jiji la Ilam, Gharb.
Lakini pia wapo wanawake waliohukumiwa kupigwa mawe, lakini wakaponea chupuchupu.
Mwaka 2002, Amina Lawal, Nigeria, alihukumiwa kupigwa mawe, lakini aliachiwa huru baada ya kukata rufaa.
Sakineh Mohammadi Ashtian alihukumiwa nchini Iran mwaka 2007, lakini hukumu yake ikapingwa na ipo katika mjadala.
Mwingine ni Safiya Husseini wa Nigeria pia, yeye aliachiwa huru baada ya kukata rufaa.
Ateseka na saratani ya mifupa kwa miaka kumi
WAKATI saratani ya matiti ikiwa tishio kwa wanawake wengi duniani, mwanamke mmoja nchini China anateseka na uvimbe mkubwa usoni mwake uliosababishwa na kuugua saratani ambao amedumu nao kwa miaka 10 sasa.
Li Hongfang (40), ameshindwa kupata matibabu ya kuondoa uvimbe huo unaomsumbua kutokana na kutomudu gharama za matibabu. Ugonjwa huo ambao umeelezwa na madaktari kuwa ni aina ya saratani ya mifupa, ni ugonjwa unaosababisha tishu kukua.
"Mimi si mtu wa kutisha, bali ni mgonjwa tu, lakini watu wengi wamekuwa wakisema kuwa ninatisha na wengine kunikimbia," anasema.
Tatizo lake lilianza mwaka 2001, wakati huo aliona kivimbe kidogo pembeni mwa kichwa chake, lakini anasema hakukitilia maanani kwani kilikuwa hakina maumivu yoyote.
Baada ya afya yake kuanza kubadilika miaka minne baadaye, madaktari walisema kuwa ana jumla ya uvimbe mdogo mdogo saba unaozidi kukua katika uso wake.
Lakini hakuweza kuwa na gharama ya kiasi cha Pauni 60,000 (zaidi ya Sh150 milioni) ili aweze kupatiwa matibabu.
"Najua kwamba watu wengi sasa wananiangalia mimi kama mtu fulani wa kutisha, lakini bado nabaki kuwa mwanamke wa kawaida na mama kwa upande mwingine," anasema.
Kwa mujibu wa madaktari, aina hiyo ya saratani huanza kukua katika fuvu la kichwa na chini ya mgongo. Ingawaje hakuna takwimu sahihi, lakini inaelezwa kuwa ugonjwa huu huathiri mtu mmoja kati ya watu milioni moja nchini Marekani.
![]() |
| Akilia kwa uchungu baada ya kueleza yanayomsibu, kama binadamu wa kawaida ni lazima ujisikie vibaya kwa jinsi watu wengine wanavyomchukulia |
Hongfang ameteseka na ugonjwa huo kwa kipindi chote hicho kutokana na mfumo duni wa matibabu na kuchelewa kupata huduma.
Wakati alipoanza kupatwa na ugonjwa huo, alikuwa akiishi na mumewe na watoto wawili katika kijiji cha Tianchao, katika Kata ya Qianxian huko Magharibi mwa China.
"Hatukuwa na fedha nyingi, lakini tulikuwa na furaha sana na tulipendana pamoja na watoto wetu wawili wa kiume. Ninaweza sema maisha yalikuwa mazuri sana, lakini kadri uvimbe ulivyozidi, aliniacha na kwenda mbali.
"Sikuwahi kufikiria kitu chochote nilipoanza kuuona uvimbe ule katika kichwa changu, nilidhani pengine ni aina tu ya wadudu walikuwa wamening'ata,” anasema.
Anaongeza: "Sikuweza kufanya lolote nilikuwa nakuna tu na kuacha lakini ilianza kukua kwa kasi.”
Nchini China, huduma za afya zinasua sua sana katika miaka ya hivi karibuni, lakini katika miaka ya nyuma kulikuwa na ada maalumu iliyotolewa katika vituo vya afya.
Hata hivyo wananchi wengi wa nchi hiyo, hawana uwezo wa kupata huduma hiyo.
![]() |
| Akionyesha picha za wanawe |
Hivi sasa China imeanza kujadili mpango wenye lengo la kutoa bima za afya kwa watu wote wanaofikia1.3 bilioni na kuazimia kuwa hadi kufikia mwaka 2020, mpango huo uwe umekamilika.
Thursday, May 17, 2012
Kwa kheri Mafisango
Marehemu akiwa nyumbani kwake enzi za uhai wake
Simanzi, huzuni na vilio viliwatawala wanamichezo nchini baada ya kupata taarifa za kifo cha kiungo wa kimataifa wa Rwanda na Simba, Patrick Mutesa Mafisango (32) aliyefariki dunia jana alfajiri kwa ajali ya gari.
Mafisango anatarajiwa kuagwa leo kwenye Uwanja TCC Sigara Chang'ombe jijini Dar es Salaam kabla ya kesho kusafirishwa kuelekea nyumbani kwao DR Congo kwa mazishi.
Msemaji wa Simba, Ezekiel Kamwaga alisema taratibu za kuuaga mwili wa marehemu zitaanza saa nne asubuhi mpaka saa 10 jioni.
Mafisango alipata mauti hayo eneo la Veta Chang'ombe usiku wa kumkia jana saa 8.45 alipokuwa akiendesha gari akitokea Maisha Club akiwa na wenzake wanne na alipofika maeneo ya Veta wakati akijaribu kumkwepa mwendesha baiskeli ya miguu mitatu 'Guta' gari lilimshinda na kugonga mti uliosababisha gari yake kuingia mtaroni na mauti kumkuta hapo hapo.
Kwa mujibu wa shuhuda wa tukio hilo mtoto wa dada yake Orly Ilemba (24) aliyekuwamo katika gari hilo alisema jana wakati wanavuka mataa ya Veta, marehemu alikuwa katika mwendo kasi mara mbele akakutana na Guta na katika jitihada za kulikwepa akagonga mti na gari kupinduka na kutumbukia mtaroni na mauti kumkuta hapo hapo.
"Tulitoka salama Maisha Club tunarudi nyumbani marehemu alikuwa akiendesha gari katika mwendo wa kasi, tulipovuka mataa ya Veta wakati akiwa 'spidi' tuliona guta kwa mbele yetu pamoja na pikipiki sasa wakati marehemu anakwepa kwa bahati mbaya aligonga mti na gari ikadumbukia ndani ya mtaro huku nikishuhudia kichwa cha ndugu yangu kikigeukia chini kwenye sehemu ya breki na miguu kuja juu kumbe tayari alishafariki......ndipo tukaanza taratibu za kumkimbiza hospitali," alisema Ilemba.
Aliongeza kuwa,"ndani ya gari hiyo aina ya Gx100 tulikuwa watu jumla ya watano mimi, Gaspar Karemera, Bozy na mwanamke mmoja ambaye yeye hatukumfahamu jina lake mara moja akiwa amekaa mbele na marehemu ambaye mpaka sasa bado yupo hospitali akiendelea na matibabu baada ya kuumia sana maeneo ya kichwani,"alisema Ilemba.
Mashabiki wa soka waliofika Kituo cha Polisi cha Chang'ombe wakiangalia gari la marehemu lililopelekwa kituoni hapo janakifo cha Mafisango
Akithibitisha kifo cha mchezaji huyo, Mkuu wa Trafiki katika mkoa wa Kipolisi wa Temeke, Prackson Lugazia alisema ajali hiyo ilitokea wakati Mafisango aliyekuwa akiendesha gari aina ya GX 100 akitoka Maisha Club akiwa na familia yake akijaribu kumkwepa mwendesha Guta.
Alisema hali hiyo ilisababisha gari hilo kuacha njia na kuingia mtaroni na kugonga miti mitatu kisha kugeuka na kuangalia lilikokuwa likitoka na baadaye kupinduka.
"Baada ya kupata taarifa za ajali hiyo majira ya saa 10 asubuhi tulifika eneo la tukio haraka iwezekanavyo, lakini hatukukuta mtu yeyote zaidi ya gari lililokuwa limepinduka,"alisema Lugazia.
Alisema,"kufuatia hali hiyo ndipo tulipoanza taratibu za kumtafuta marehemu na tulianzia hospitali ya Amana, tulikwenda hospitali ya Mwananyamala na baadaye Muhimbili ambako tuliukuta mwili wake pamoja mwanamke mmoja ambaye alikuwa na majeraha mbalimbali sehemu za mwili wake," alisema Lugazia.
Akizungumza jana alfajiri jijini Dar es Salaam Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage alisema,"ni kweli Mafisango hatunaye tena, kwa sasa siwezi kuzungumza chochote huyu ni mchezaji wa timu ya Taifa ya Rwanda, ndiyo nafanya mawasiliano na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) na lile la Rwanda (FERWAFA) kuangalia namna ya kuusafirisha mwili wake."
Mafisango amefariki akiwa amemaliza mkataba wake na Simba na alitarajiwa kusaini mkataba mpya juzi na leo alitarajiwa kwenda Rwanda tayari kujiunga na kikosi cha timu hiyo 'Amavubi' kinachojiandaa kwa ajili ya mechi za mchujo za kuwania kufuzu Fainali za Kombe la Dunia 2014, zitakazochezwa mwezi ujao.
| Baadhi ya wasanii na wachezaji waliofika Hospitali ya Muhimbili kupata uhakika wa kifo cha Mafisango |
"Ukiniambia amefariki sikuelewi hapa nilipo nimechanganyikiwa, kuna vikao vinaendelea (jana), nitakupigia baadaye,"alisema Micho huku sauti yake ikionekana kuwa na majonzi.
Wakati huohuo; Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limepokea kwa masikitiko kifo cha mchezaji wa Simba na timu ya Taifa ya Rwanda (Amavubi), Patrick Mafisango kilichotokea leo (jana) alfajiri kwa ajali ya gari Dar es Salaam.
TFF ilisema msiba huo ni mkubwa kwa familia ya mpira wa miguu kwani Mafisango kwa kipindi chote alichocheza mpira hapa nchini akiwa na timu za Azam na baadaye Simba, aliifanya kazi yake (kucheza mpira) kwa bidii.
Kifo chake ni pigo kubwa sio tu kwa familia yake na timu alizochezea, bali Ukanda mzima wa Afrika Mashariki na Kati ambapo changamoto za Mafisango zilikuwa dhahiri uwanjani.
BOBAN
Rafiki mkubwa wa Mafisango kiungo Haruna Moshi 'Boban' alikuwa kwenye majonzi makubwa huku machozi yakimtoka bila kuzungumza lolote.
Wakizungumzia ukaribu wa mchezaji huyo na marehemu baadhi ya wachezaji wa Simba walidai Boban ndiye alikuwa rafiki mkubwa wa Mafisango na walikuwa kila mara wakiongozana pamoja katika starehe na hata wakiwa kambini.
![]() |
| Boban |
"Boban ndio alikuwa mtu wa kwanza kusambaza habari za kifo cha Mafisango kwetu na hata aliposikia taarifa hizo alichofanya alikwenda moja kwa moja Muhimbili kwenye chumba cha maiti na kuomba kuonyeshwa mwili wa marehemu na baada ya hapo hakuzungumza lolote mpaka hapa mnavyomuona,"alisema Juma Jabu.
Mafisango alijiunga na Simba akitokea Azam Fc, mwaka jana alizaliwa Machi 7, mwaka 1987, nchini Rwanda na alikuwa akiichezea timu ya Taifa ya nchi hiyo kabla ya kusimamishwa kwa muda mrefu kutokana na utovu wa nidhamu na amerudishwa kundini na kocha Micho, lakini hata hivyo hajaweza kuitumikia timu hiyo ya Taifa lake.
Mchezaji huyo atakumbukwa kwa mchango wake mkubwa katika timu ya Simba msimu huu uliomalizika hivi juzi na kung'aa zaidi katika Ligi hiyo kwa kupachika mabao na kutoa pasi za mwisho, ambapo Mechi ya mwisho ya Mafisango ilikuwa ni kati ya Simba dhidi ya Al Ahly Shandy Jumapili katika hatua ya 16 Bora ya Kombe la Shirikisho, ambayo Simba ilitolewa kwa penati 9-8, kufuatia sare ya jumla ya mabao 3-3.
Wakati mechi ya kwanza kati ya Simba na Wasudan hao iliyochezwa hapa nyumbani kwenye Uwanja wa Taifa, Mafisango aliifungia timu yake bao moja kati ya matatu yaliyoiwezesha Simba kuibuka na ushindi wa mabao 3-0 katika mchezo huo.
Monday, May 14, 2012
Baada ya kazi kubwa sasa ni kusherehekea kwa kwenda mbeleee!
Baada ya miaka 50 ya Uhuru
Umewahi kuiona hii??!! Hakunaga!
Tamwa yawapa somo wakuu wapya wa Wilaya
Shakila Nyerere
Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania(Tamwa), kimewataka Wakuu wa Wilaya walioteuliwa kuwa makini katika ufuatiliaji wa Watendaji wa Halmashauri katika shule za kata kuepukanana mimba na kufeli kwa wanafunzi wa kike nchini.
Akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa Tamwa, Ananilea Nkya alisema wakuu wote wa Wilaya walioteuliwa wawe ni mifano kwa viongozi wengine walioko madarakani kufuatilia majukumu yanayozikabili jamii.
Alisema kwa takwimu walizozifanya kwa kushirikiana na wanahabari kupata takwimu hizo zilizohusu shule za kata katika mikoa 20 Bara na Visiwani kwa kila Wilaya moja katika Kata mbalimbali kwa shule 7 hadi 10 walibaini kuwa idadi kubwa ya wanafunzi wanoacha shule au kufeli ni wanafunzi wa kike.
Nkya alisema mazingira ya shule zilikojengwa ni hatari kutokana na kukosekana kwa mahitaji muhimu kwa wanafunzi kama vile Maji, miundombinu mibovu ya barabara ni sababu mojawapo ya kuwapa vishawishi wanafunzi wa kike kuishi wakidanganyika kwa kupitia udhaifu wa maisha waliyonayo.
“Wakati mwingine wanafunzi wa kike hulazimika kuishi kwa Walimu wa kiume na kuwa na mahusiano ya kimapenzi kinyume na maadili na sheria na wengine hujikuta wakiishi kwa vijana walioko mitaani kwa kutaka kujikimu kimaisha na kupata mahitaji ya kujikidhi wanapokuwa shuleni, hiyo yote ni hali za shule za kata kuwa na mapungufumengi,” alisema Nkya.
Nkya aliongeza kwa kusema mazingira ya shule za kata zilizoko mikoani na wilayani kwa upande wa walimu ni matatizo makubwa sana maana inafikiwa wakati mwingine shule yenye kidato cha kwanza hadi cha sita kuwa na walimu watatu ikiwa mwalimu wa somo la sayansi ni mmoja na kwingineko hakuna kabisa mwalimu wa somo hilo la sayansi.
Walimu walioko wanaofundisha somo la sayansi ni mwalimu wa somo la sanaa ndiye anayefundisha sayansi kataka shule hizo.
“Ili taaluma ikue nchini hapa kinachotakiwa ni kuboresha mahitaji muhimu ikiwemo miundombinu kwa walimu na wanafunzi ikiwa ni pamoja na uwajibikaji wa viongozi kutoa ushirikiano wa kutosha kwa kufuatilia watendaji katika idara zao.”
Aliongeza kwa kusema wanafunzi wa kike hufeli na kukatiza masomo kwa kubeba mimba shuleni ni pamoja na kukosekana kwa walimu ambao kwa asilimia 80 wamekuwa wakishindwa kuwasili katika vituo vya kazi wanavyokuwa wamepangiwa wakikumbana na mazingira magumu kwa mara ya kwanza.
Pale ubora unapoonekana
Sunday, May 13, 2012
Magari ya kifahari bado yamtoa udenda Cristiano Ronaldo, ayajaza manane uani kwake
Kuwa mwanasoka ghali duniani kunafanya pesa lisiwe tatizo lako la msingi. Ni kama ilivyo kwa staa wa Real Madrid, Cristiano Ronaldo. Tajiri huyu kijana ananunua chochote anachojisikia kwa sasa.
Kwa mujibu wa mkataba wake, Ronaldo, analipwa kiasi cha Euro 12 milioni kwa mwaka na Real Madrid. Hii ni achilia mbali mikataba mbalimbali ya kibiashara ambayo inamwingizia mabilioni ya pesa yanayomfanya awe miongoni mwa wanasoka wanaoingiza pesa nyingi zaidi duniani kwa sasa.
Hata hivyo, ugonjwa wake wa kupenda magari ya kifahari umemfanya Ronaldo ajaze magari mengi ya bei mbaya uani kwake. Amekuwa akiyatumia mara kwenda mazoezini na katika matembezi binafsi.
Yafuatayo ni magari manane ya kifahari ambayo Ronaldo ameyajaza uani na ambayo huwa anayaendesha mara kwa mara.
Bugatti Veyron
Hili ndilo gari kipenzi la Ronaldo. Bugatti Veyron ni ghali zaidi na lina mwendo wa kasi zaidi duniani. Mwendo Kasi wake wa juu huwa unafikia kilomita 407 kwa saa na linaweza kumpita dereva wa formula one anayeendesha kwa kilomita 360. Staa wa Cameroon, Samuel Eto’o ni mchezaji mwingine anayemiliki gari la aina hiyo.
Bugatti huwa linauzwa kwa oda maalumu kutoka kiwandani na mhusika analazimika kulisubiri kwa kipindi fulani wakati likitengenezwa. Linauzwa kiasi cha dola 1.2 milioni na hivyo kulifanya kuwa gari ghali zaidi duniani kwa sasa.
Rolls-Royce Phantom Drophead Coupe
Rolls-Royce ni gari linaloheshimika zaidi Uingereza. Gari hili linamilikiwa na watu matajiri. Kuna watu wachache sana wanaomiliki gari hili Uingereza. Lina thamani ya dola 443,000 za Marekani.
Kinachoshangaza ni kwamba nyuma ya gari hili unaweza kufungua katika sehemu ya mizigo na kupata eneo la kukaa kufanya pikiniki.
Ukifungua kuna meza inajipandisha na kuna sehemu za kuwekea vinywaji mbalimbali.
Porsche Cayenne Diesel
Gari hili limetoka Mei mwaka huu na Ronaldo alilisubiri kwa muda mrefu kulinunua moja kwa moja. Lina injini yenye nguvu na kasi yake ni kilomita 218 kwa saa. Kwa suala la mafuta, gari hili lina uwezo wa kutumia lita 10 kwa mwendo wa kilomita 100. Hili ni moja kati ya magari ya bei rahisi ambayo Ronaldo anayo. Lilimgharimu kiasi cha Euro 49,000.
BMW M6
Duniani kote gari hili linatambulika kuwa ndoto ya kila mtu anayetaka kuendesha ‘Sports Car’. Kwa Ronaldo, hili ndilo gari linalomfaa zaidi kwa sababu yeye ni mwanamichezo wa hali ya juu.
Ingawa bei yake ni dola 100,000, Ronaldo hakuona shida kulinunua na kulitupia uani kwake. Ni moja kati ya magari anayotumia sana.
Porsche 911
Ni moja kati ya magari ya kifahari duniani kote. Lilimgharimu Ronaldo kiasi cha euro 201, 682 kuliweka uani kwake. Ni moja kati ya magari anayoyatumia mara kwa mara pia akienda katika starehe zake.
Bentley Continental GT
Hili ni moja kati ya magari yenye nguvu ambayo kampuni ya Bentley imewahi kuyatengeneza. Gari hili pia lina kasi kubwa huku likitumia mwendo wa kilomita 320 kwa saa. Kutokana na mapenzi yake kwa gari hili, Ronaldo alilazimika kutumia kiasi cha dola 375,000 za Marekani kwa ajili ya kulinunua na kuliweka uani kwake. Ni gari la kifahari ambalo ni ndoto ya wengi.
Ferrari F430
Gari hili la siti za watu wawili tu. Kwa sasa ndiyo dili na Ronaldo bado ana mapenzi nalo ya dhati.
Kuna watu wanasema lishastaafishwa lakini Ronaldo hakutaka kuliuza na mpaka leo amekuwa akilitumia mara nyingi. Alitumia kitita cha dola 188,000 za Marekani kulinunua.
Audi R8
Moja kati ya magari yenye kasi duniani. Gari hili lina uwezo wa kukimbia kwa kilomita 316 kwa saa. Kwa kuliweka uwani kwake kukamilisha idadi ya magari manane ya kifahari aliyonayo, Ronaldo alilazimika kujikamua kiasi cha dola za Marekani 109,000 ili kulinunua.
Subscribe to:
Posts (Atom)





























